31 May 2013

Viongozi Newala wafurahishwa na vikundi vya wakulima



 USHIRIKIANO na mwamko wa wakulima walioungana katika vikundi kutekeleza mradi wa Mpango wa Maendeleo vijijini; katika mwambao wa Pwani ya Tanzania (CRSPT); unaotekelezwa na Aga Khan Foundation, katika Wilaya ya Newala, umewafurahisha, viongozi katika kata ya Mcholi ya kwanza, walioshiriki siku ya wakulima kijijini, Chiunjila, anaripoti Godwin Msalichuma, Newala.
Hayo yalijitokeza kijijini hapo hivi karibuni, ambapo diwani Selemani Kaisi, alipopewa fursa ya kuzungumza na vikundi vya wakulima takribani 87, wanaume 61 na wanawake 26, walikusanyika katika siku yao, ili kujifunza pamoja mambo muhimu na changamoto zinazowakumba katika mradi huo wa kilimo cha mpunga na ufuta.
“Nimeridhishwa sana na utekelezaji wenu wa mradi huu kwa ushirikiano na kwa kweli unanitia moyo kuona haya yakifanyika kwa umoja na nguvu ya pamoja, niseme kuwa mmeshakuwa wataalamu sasa, ninaimani mnaweza kuendelea hata bila ya wafadhili kuwepo” alisema Kaisi na
kuongeza kwa kuwaasa:
Waendelee na utaalamu huo walioupata kuboresha kilimo cha mpunga na ufuta na pia kuhifadhi elimu hiyo kwa faida ya vizazi vyao vijavyo.
Alisema, amefurahishwa na kusikia kuwa awali kabla ya mradi wakulima walikuwa wanavuna mpunga katika hekta moja magunia manne mpaka matano, lakini sasa wanafikisha magunia 25 mpaka 40.
Aidha, aliwaomba kuwa macho na walanguzi wa mazao wakati wa mavuno; kwani mbinu wanazopewa na asasi hiyo ya kimataifa, ni nzuri ya kukusanya na kuhifadhi pamoja, wakisubiri bei nzuri itakapofika katika zao hilo la mpunga.
“Nawaomba muwe macho na walanguzi wa mazao yenu, wasije wakawarubuni wakati wa mavuno tukauza mpaka mbegu; nawasihi mtumie hivyo vikundi vya kuweka na kukopa (Vicoba), yaani ‘wekeza boresha maisha’ hapo tukiweka akiba nadhani kilimo kitakuwa na manufaa zaidi,” alisema diwani huyo.
Naye, Ofisa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo katika Wilaya ya Newala (DALDO), Alford Mpanda, alisema, baada ya kuona maendeleo mazuri ya kilimo cha mpunga kijijini Chiunjila, alidai amegundua kuwa kumbe kuna mazao ambayo wakulima, wanaweza kuzalisha bila mikikimikiki kama ilivyo kwa zao la korosho, ambapo lina gharama kubwa katika kuandaa shamba na kupata mapato yake.
“Inanipa moyo sana na nguvu kuona kuwa kumbe kuna mazao kama mpunga na ufuta yanachukua muda mfupi na gharama ndogo k u y a z a l i s h a , h a t a h a k u n a mikikimikiki ukilinganisha na zao la korosho,” alisema Mpanda.
Hata hivyo alifurahishwa na kuridhishwa kuona kuwa hata mapato kwa wakulima yameongezeka kutoka magunia matano kwa hekta mpaka magunia 40, ambapo aliwashauri kuongeza bidii katika uzalishaji, kwani pia uzalishaji wao unaongeza pato la halmashauri na Taifa kwa ujumla wake.

No comments:

Post a Comment