18 May 2013

Polisi Dar wakamata milipuko ya mabomu

Darlin Said na Leah Daud


 JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linawashikilia watu watano kwa kukutwa na milipuko hatari ya mabomu ambayo walikuwa wakiimiliki kinyume cha sheria.
 Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Kamanda wa kanda hiyo, Suleiman Kova, alisema watuhumiwa hao wamekamatwa katika msako unaoendelea jijini humo.
Alisema katika msako huo, jeshi hilo limekamata nyaya 62 za milipuko
zikiwa zimefungwa betri na vifaa vya kusababisha mlipuko ambavyo vyote vikiunganishwa, vitatoa mlipuko mkubwa unaoweza kuangusha ghorofa, kuua na kuharibu mali.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Bw. Juma Khalifan (24), Bw. Ruben Patrick (26), Bi. Happy Charles (28), Bw. Sadick Seif (32) na Bw. Idd Shabani (40) ambao walikamatwa eneo la Kunduchi Mtongani baada ya jeshi hilo kupata taarifa za raia mwema.
Alisema pamoja na kukamata milipuko hiyo, pia wamekamata gari aina ya Noah yenye namba T 772 BYC pamoja na pikipiki aina ya Bajaj yenye namba T959 BTE zilizokuwa zikitaka kusafirisha milipuko hiyo kutoka nyumba kwa Bw. Seif.
“Mara nyingi milipuko hii inatumika kwenye shughuli za uvuvi na migodini ila cha ajabu zaidi, watuhumiwa hawa si wavuvi wala hawamiliki migodi,” alisema Kamanda Kova.
Aliongezea kuwa, kutokana na hali hiyo jeshi hilo limepatwa na mashaka juu ya watu hao kumiliki milipuko na wapi walikuwa wanaipeleka hasa ukizingatia kuwa, yapo matukio mbalimbali yanayoendelea kutokea nchini.
Alisema jeshi hilo linaendelea kuwahoji watu hao kabla ya kufikishwa mahakamani.

No comments:

Post a Comment