18 May 2013

Mwakyembe aliteka Bunge


*BAJETI YAKE YAPITA, ABAINI WIZI VITUO VYA MALIPO
*AWATAKA POLISI KUZIACHIA NOAH WALIZOKAMATA
*KIGWANGALLA AIHADHARISHA CCM UCHAGUZI 2015

Goodluck Hongo na Darline Said


 SERIKALI imetoa agizo la kufungwa mara moja kwa ofisi zinazotumika kubadilisha makadirio ya fedha ambazo hutakiwa kulipwa na wafanyabiashara katika Ofisi za Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), zilizopo Keko na Lumumba, Dar es Salaam.
Vituo hivyo hutumika kubadilisha kiasi cha fedha ambacho hupaswa kulipwa TRA ili kugomboa mizigo yao kwenye Bandari ya Dar es Salaam.
Agizo hilo limetolewa bungeni Mjini Dodoma jana na Waziri wa Uchukuzi, Dkt. Harrison Mwakyembe, alipokuwa akijibu maswali ya wabunge wakati akihitimisha mjadala wa makadirio ya bajeti ya
Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2013/14.
Alisema wapo baadhi ya watu ambao wanaitumia Bandari ya Dar es Salama kama mashine ya kutolea fedha (ATM), na kujinufaisha wakishirikiana na baadhi ya wafanyakazi.
Aliongeza kuwa, yeye ameingia mkataba na Rais Jakaya Kikwete ili kufanikisha malengo ya Serikali na kama atashindwa kuyafikia malengo hayo afukuzwe hivyo hayupo tayari kubeba lawama wakati watu wanaosababisha uzembe wanaweza kuondolewa na kupisha wengine wafanye kazi hizo.
Dkt. Mwakyembe alisema kwa sasa Serikali haina mzaha na mtu ambaye atakwepa kulipa kodi au kufanya udanganyifu katika mfumo mpya wa kulipia kodi.
“Nawaonya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari (TPA), Mkurugenzi Mkuu wa Fedha na Mkurugenzi wa IT, kuanza kutumia mfumo mpya wa malipo ili kudhibiti mapato ya bandari.
“Kama watashindwa, hatutasita kuwafukuza mara moja kwani Bandari ya Dar es Salaam ndiyo inayotakiwa kuingiza mapato makubwa makubwa serikalini,” alisema Dkt. Mwakyembe.
Aliwataka wabunge na wananchi kufanya uchunguzi wa kina ndipo wahoji kwa nini Serikali imeamua kujenga Bandari ya Bagamoyo, mkoani Pwani.
“Hatukufanya hivi kwa sababu ya Rais Kikwete ila kutokana na hali ya kuelemewa...baada ya miaka mitatu ijayo Bandari ya Dar es Salaam itaelemewa kwa mizigo ambayo nchi ya Burundi inatarajia kusafirisha madini ya nikeli zaidi ya tani milioni tatu hivyo ni lazima kuwepo na mbadala wa bandari,” alisema.
Aliongeza kuwa, wafanyakazi wote wa Wizara hiyo lazima wafanye kazi zao kwa uadilifu ambapo kipaumbele cha Wizara na Serikali ya awamu ya nne ni kujenga reli mpya nchi nzima kwa ubora zaidi.
Alisema ili aweze kutimiza malengo yake, hatamuonea huruma mtu yeyote ambaye atakwenda kinyume na maadili ya kazi yake ndio maana anaendelea kusafisha kila sehemu.
Dkt. Mwakyembe alisema viongozi wa Shirika la Ndege nchini, (ATCL), wameacha deni kubwa ambalo walilipia ndege iliyokuwa kwenye matengenezo hivyo lazima kuwepo na utaratibu wa kuwajibishana kabla ya kulirudisha katika hali ya kawaida.
“Si kwamba nchi kama Burundi au Rwanda zinatushinda katika sekta hii bali kilichopo ni kwamba, kupanga ni kuchagua wao wamechagua ndege na sisi tumechagua barabara,” alisema.
Akizungumzia magari aina ya Noah kubeba abiria, aliitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Usafiri Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), kuzungumza na watu wenye magari ili kuona uwezekano wa kufanya kazi ya kubeba abiria kwani wote ni Watanzania ambao tunajenga nchi moja.
“Naliagiza Jeshi la Polisi kuyaachia mara moja magari yote aina ya Noah ambayo yamekamatwa na yapo kituoni bila masharti, watu wote wenye taarifa ya kutakiwa kulipia mizigo kwa dola badala ya fedha za Tanzania, nileteeni majina ya watu hao ili niweze kuchukua hatua za haraka,” alisema.
Dkt. Kigwangalla
Katika hatua nyingine, Mbuge wa Nzega, mkoani Tabora, Dkt. Hamisi Kigwangalla, amekihadharisha Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuwa makini na Uchaguzi Mkuu wa 2015, kutokana na Mkoa huo kuwa nyuma kimaendeleo.
Dkt. Kigwangalla aliyasema hayo bungeni mjini Dodoma jana wakati akichangia mjadala wa bajeti ya Wizara hiyo.
Alisema Mawaziri wote wanatoka CCM lakini anashangaa kuona Mkoa huo umesahaulika hivyo kutoa mwanya kwa wapinzani kutumia fursa hiyo kukichafua chama chao.
Aliongeza kuwa, vyama vya upinzani vinapokuwa katika mikutano ya hadhara huwaambia wananchi kuwa hawapati maendeleo kutokana na kuichagua CCM hivyo lazima Mawaziri wautazame Mkoa huo ili kujiwekea mazingira mazuri ya ushindi 2015.
“Siungi mkono bajeti ili Waziri afanye kazi vizuri...nilisafiri na Waziri hadi jimboni kwake mkoani Mbeya kwa barabara ya lami lakini kutoka Dodoma hadi Tabora ni kilomita kama 400 lakini ukifika mgongo unauma kutoka na ubovu wa barabara,” alisema.
Akizungumzia usafiri wa anga, Dkt. Kigwangalla alisema ni aibu kwa Tanzania kukosa ndege hata moja inayokwenda nje ya nchi ambapo hali hiyo inatokana na uongozi mbovu si vinginevyo kwani Wachina wakitumika vizuri wataleta maendeleo nchini.
Alisema China ni rafiki mzuri wa Tanzania hivyo Serikali inaweza kuzungumza nao ipewe mkopo au kuzungumza na kampuni kubwa zinazotengeneza ndege na kuingia nao mkataba ili kuwepo na safari za nje ya nchi.
Hata hivyo Bunge lilipitisha Bajeti ya Wizara hiyo zaidi ya sh. bilioni 491.

2 comments:

  1. Masuala ya TRA kwa kweli yanaudhi! Kwa mfano ukihitaji huduma katika ofisi za TRA (Moshi) ukaenda mwenyewe, utazungushwa - njoo baadaye, njoo kesho, kesho kutwa....! Lakini ukiwatumia "vishoka" au waajiriwa WA WAFANYAKAZI WA TRA, ambao wako hapo nje tu kwa wingi (bila vitambulisho) mambo yako yatakuwa ni kufumba na kufumbua umepata risit au huduma unayoihitaji. Kama ndivyo kwanini serikali isihalalishe VISHOKA na kututangazia rasmi kwamba hatuwezi kupata huduma katika ofisi hizi (TRA) bila kupitia kwa VISHOKA???

    ReplyDelete
  2. Ni kweli kabisa hili kuhusu VISHOKA! Hata mimi mwaka jana nilikuwa hapo moshi katika ofisi za TRA kulipia Road License ya gari yetu ya nyumbani! Nilitumwa kwenda benki, unga folen, lipia huko alafu ndo uje! Kwanza niliulizwa, "Nani kakutuma hapa?" Katika kushangaa na kuuliza "wanaujua mji" niliambiwa tumia KISHOKA! Baada ya kuongea na jamaa mmoja akaniambia nimpe Shs. 10,000/= na hizo karatasi zangu. Nikakaa hapo nje kusubiri na kabla sijamaliza coca cola moja nikaletewa risit za malipo na kila kitu kikiwa tayari! Nikaambiwa nirudi kesho kutwa yake kuchukuwa stika! Tukienda hivi, sisi Watanzania tutafika? TRA!TRA!TRA!TRA!TRA!TRA!TRA! sikilizeni kilio chetu!!

    ReplyDelete