31 May 2013

Minazi, karafuu yahamia Wizara ya Kilimo

Na Mwajuma Juma,  
 MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali amesema kuwa kuanzia sasa mashamba yote ya karafuu na minazi yaliyokuwa chini ya usimamizi wa Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati yatakuwa yakishughulikiwa na Wizara ya Kilimo na Maliasili, ili kuondoa mvutano wa kiutendaji baina ya wizara hizo mbili.
Balozi Seif alitoa uamuzi huo katika Chuo cha Amali vitongoji Chake Chake Pemba wakati akizungumza na masheha wa mikoa miwili ya kisiwani Pemba.
Alisema udhibiti wa mapato yanayotokana na mazao yaliyomo kwenye baadhi ya mashamba ya Serikali yalikuwa yakileta mgongano kutokana na mashamba hayo kushughulikiwa na Wizara mbili tofauti.
Hivyo aliwaomba Masheha ambao maeneo yao yamo mashamba ya
Serikali ya karafuu na minazi na hadi sasa hayajahakikiwa watoe taarifa kwa Ofisa Mdhamini wa Wizara ya Kilimo Pemba au kiongozi yeyote atakayewekwa kwenye kanda hiyo.
Akizungumzia suala la udhibiti wa ukataji ovyo wa misitu,Balozi Seif aliwakumbusha Masheha hao kuhakikisha kwamba wimbi la ukataji ovyo wa miti unadhibitiwa.
'Kijani ya Pemba tunataka ibakie kama kawaida na hili litafanikiwa iwapo wana jamii pamoja na masheha watashirikiana katika udhibiti wa ukataji ovyo wa misitu' alisisitiza Balozi Seif.
Wakielezea changamoto zinazowakabili baadhi ya Masheha hao walisema mazingira duni wakati wanapostaafu utumishi wao pamoja na mfumuko wa hujuma wanazofanyiwa masheha limekuwa tatizo kubwa linalopunguza ari ya utekelezaji wa majukumu yao.
Masheha hao waliiomba Serikali Kuu kujenga mazingira yatakayowawezesha kupatiwa mikopo ya vyombo vya usafiri ili kurahisisha kazi zao masuala ambayo Balozi Seif aliahidi kwamba Serikali itayazingatia na kuyapatia ufumbuzi unaofaa.

No comments:

Post a Comment