30 May 2013

Mbunge amkingia kifua JK bungeni

Na Waandishi Wetu


 MBUNGE wa Peramiho kwa tiketi ya CCM, Jenista Mhagama , amemkingia kifua, Rais Jakaya Kikwete, akitaka Bunge lisimfanyie tathmini kuhusiana na kauli yake kuwa hali ya kifedha kwa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii nchini ni nzuri, kauli ambayo kambi rasmi ya upinzani bungeni, imedai inapingana na ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ambayo imeonesha hali ya mifuko hiyo kuwa ni mbaya
 Mbunge huyo alitoa kauli hiyo bungeni mjini Dodoma jana, wakati akichangia makadirio ya bajeti ya Wizara ya Kazi na Ajira kwa mwaka wa fedha 2013/14.
Alisema kuwa kitendo cha kumpakazia maneno Rais Kikwete, si jambo la
heshima hata kidogo na hata kama amesema kweli au hapana tumwache afanye kazi.
“Hatuwezi kusema tumfanyie tathmini Rais katika Bunge hili, hili si suala la heshima hata kidogo kwani baba hawezi kutoa siri ndani ya nyumba yake, lakini Rais Kikwete ameeleza wazi kuhusu mifuko hiyo, hili ni jambo la kumpongeza,” alisema.
Alisema anaipongeza Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwani inafanya kazi yake vizuri na kutaka viongozi wa mifuko hiyo kuendelea kuchapa kazi bila kubabaishwa.
“Halima (Mdee) hapa tulipo kwenye jengo hili limejengwa na mifuko hii, Chuo Kikuu cha UDOM wanaposoma wadogo zako kimejengwa na mifuko hii, sasa mnaposema hamuoni kazi mnataka kurudisha nyuma maendeleo?” alihoji.
Kwa upande wa ajira, alisema ni lazima kijipanga kutafuta suluhu na si kubaki kufurahia wawekezaji katika nchi yetu. Alisema kabla wawekezaji hawajafika nchini, waulizwe wataajiri vijana wasomi wangapi, wataje vijana wa elimu ya kati wangapi na vibarua wangapi, ili ijulikane.
Aliongeza kuwa Wizara inatakiwa kuangalia hali ya wafanyakazi kwenye sekta binafsi, kwani wengi wao wanaajiriwa bila kuwa na mikataba na migogoro mingi inatokea katika sekta hizo kutokana na mishahara duni.
Awali kabla ya Mbunge, Mhagama kuanza kuchangia msemaji wa kambi rasmi ya upinzani bungeni, Cecilia Paresso, akiwasilisha hotuba ya kambi hiyo, alisema mifuko hiyo ipo katika hali mbaya kulingana na na ripoti ya CAG.
Alisema ripoti hiyo ya CAG ilionesha mifuko ya hifadhi ya jamii iko katika hali mbaya kutokana na kudai zaidi ya trilion 6.4 fedha ambazo hazilipiki.
“Mfano PSPF ilitoa kiasi cha sh.bilioni 67 ambazo hazilipiki, ambapo moja ya kampuni ambazo zilipewa fedha hizo zisizolipika ni pamoja na kampuni ya Tanpower Resources ya makaa ya mawe inayomilikiwa Benjamin Mkapa na Daniel Yona, ambayo ilipewa sh. bilioni 5.4,” alisema Paresso.
Aliongeza kuwa kauli ya Rais Kikwete wakati wa Maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Mei Mosi kuwa hali ya mifuko hiyo ni nzuri inaonekana kutofautiana na ripoti ya CAG ambayo inaonesha hali ya mifuko hiyo ni mbaya.
“Kutokana na kauli hizo mbili ya Rais na CAG wananchi wanamuamini nani? Ni nani anayetoa taarifa sahihi juu ya mifuko hiyo? Tumwamini Rais au CAG? Upi ni ukweli!” Alihoji Paresso na kuongeza kuwa serikali isitishe mara moja miradi ambayo fedha zake hazilipiki.
Naye Mbunge wa Viti maalumu (CHADEMA) ,Christowaja Ntinda alisema kuwa serikali iache tabia ya kugeuza mifuko ya hifadhi za jamii kama ATM yao ya kutolea fedha na kushindwa kulipa madeni yao.
Imeandikwa na Grace Ndossa Gladness Theonest, Goodluck Hongo.

No comments:

Post a Comment