31 May 2013

'Majambazi' wasomewa mashtaka hospitalini

Na Said Hauni, Lindi


 WAKAZI wawili katika Halmashauri ya Manispaa ya Lindi,wamefikishwa mahakamani wakikabiliwa na shtaka la kujihusisha na masuala ya ujambazi kwa kutumia silaha mbalimbali ikiwemo bunduki ya kienyeji na kufanikiwa kupora bidhaa na fedha taslimu jumla ya sh milioni 1.2.
Washtakiwa hao ambao kesi yao ipo kwa Hakimu Aluu Nzowa wa Mahakama ya wilaya hiyo ni, Hamisi Athumani Mbuhi na Rajabu Juma Ndete wote ni wakazi wa mtaa wa Kongo mjini Lindi na wamelazwa hospitali ya mkoa huo Sokoine.
Akiwasomea shtaka lao katika wodi namba sita walikokuwa wamelazwa Mwanasheria wa
 Serikali, Juma Maige alidai Mei 20 mwaka huu usiku washtakiwa wote kwa pamoja walifika dukani kwa Hamisi Hassani Bakari lililopo Kijiji cha Mkwajuni Wilaya ya Lindi na
kupora bidhaa na fedha taslimu.
Maige aliiambia mahakama hiyo kwamba siku hiyo washtakiwa wakiwa na bunduki moja aina ya Shotgun iliyofutwa namba zake pamoja na panga walifanikiwa kupora simu sita za mkononi za watu waliozipeleka kwa ajili ya kuchaji na fedha taslimu Sh.900,000/-na kufanya jumla ya sh.milioni 1.2.
Alidai mahakamani hapo kwamba siku hiyo washtakiwa wakiwa na silaha hizo walifika dukani kwa mlalamikaji huyo na kuanza kupiga risasi hewani ikiwa na lengo la kutisha majirani wasitoke nje nyumba zao kisha kuvunja mlango
 wa duka lake na kupora bidhaa na fedha hizo na kutoka nazo nje ambapo waliendelea kupiga risasi hewani hadi kuishiwa.
Mwanasheria huyo wa Serikali alidai kwamba washtakiwa wamefanya kosa chini ya kifungu cha 287 kanuni ya adhabu sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2002.
Pia aliiambia mahakama hiyo kwamba kitendo cha watuhumiwa hao kuishiwa risasi kwenye bunduki yao kulitoa mwanya kwa wananchi ambao walijitokeza na kufanikiwa kuwatia mikononi na kuanza kuwapiga hadi kuishiwa nguvu.
Alidai kitendo cha kuishiwa nguvu kuliwafanya wananchi hao kuendelea kujichukulia sheria mikononi ikiwemo kuwafunika nyasi na kuwachoma moto kabla ya kuokolewa na Polisi waliofika kijijini hapo muda mfupi.
Washtakiwa wote kwa pamoja wamekana shtaka lao na kesi yao,namba 49/2013,imepangwa kusikilizwa tena mahakamani hapo Juni 06 mwaka huu na wote wapo chini ya uangalizi wa askari magereza katika hospitali ya Sokoine.

No comments:

Post a Comment