15 May 2013

CUF: Saudi Arabia iombwe radhi

David John na Neema Malley


 CHAMA cha Wananchi (CUF), kimeitaka Serikali itoe tamko la kuiomba radhi Serikali ya Saudi Arabia kutokana na raia wake wanne kuhusishwa na tukio la ulipuaji bomu mkoani Arusha na baadaye kuachiwa baada ya uchunguzi kubaini hawakuhusika.
Tukio hilo lililotokea Mei 5 mwaka huu, katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, mkoani humo ambapo watu watatu walifariki dunia na wengine zaidi ya 60 kujeruhiwa.
Mwenyekiti wa chama hicho Taifa,
Prodesa Ibrahim Lipumba, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akifungua Kikao cha Baraza Kuu la chama hicho na kuongeza kuwa, kwa muda mrefu Saudi Arabia na Tanzania zimekuwa na uhusiano mzuri hivyo ni wajibu wa Serikali kuomba radhi ili kuendeleza uhusiano huo.
Alisema wageni hao waliingia nchini kihalali hivyo kitendo cha kuhusishwa na tukio hilo ambalo limetangazwa katika vyombo mbalimbali vya habari kimechafua jina la nchi yao.
“Serikali inapaswa kuwa makini na inachokifanya, kitendo cha kuwakamata wageni hawa ambao wanatoka kwenye nchi ya Kiislamu, kinaweza kuwagawa Waislamu na Wakristo kitu ambacho ni hatari kwa Taifa,” alisema.
Aliongeza kuwa, Serikali inatakiwa kuchukua hatua stahiki yanapotokea matukio makubwa kama hilo la uvunjifu wa amani ili kuwajengea imani Watanzania kuwa Serikali yao ipo makini.
Katika hatua nyingine, Prof. Lipumba alizungumzia uamuzi wa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam, kumuachia huru Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Shekhe Ponda Issa Ponda.
Alisema kilichofanywa kwa kiongozi huyo si cha kiungwana kwani kesi iliyokuwa ikimkabili ilikuwa ikihusu kiwanja hivyo ingehamishiwa kwenye Mahakama ya Ardhi.
“Serikali imekuwa ikikuza mambo na kusababisha mifarakano katika jamii...inapaswa kufanya uchunguzi wa kina kwanza kwani mwisho wa siku nchi itaingia katika matatizo,” alisema.
Pia Prof. Lipumba alidai kuhofia deni kubwa la Taifa na kudai kuwa ili kuondokana na madeni ya aina hiyo, Serikali inapaswa kuacha tabia ya kukopa bila utaratibu kwani mwisho wa siku tutashuhudia Taifa likipata mzigo wa kurejesha madeni hayo.
Aliongeza kuwa, kipindi cha utawala wa Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Bw. Benjamin Mkapa, wakati akiingia madarakani alikuta Taifa likiwa na deni kubwa hivyo alitumia kipindi cha miaka mitano kulipunguza sana.
Alisema pamoja na nchi kuwa na rasilimali za kutosha katika Taifa, bado utegemezi umekuwa mkubwa na Serikali imekuwa bingwa wa kutoa ahadi za kutekeleza miradi mbalimbali.

No comments:

Post a Comment