05 April 2013

Waziri Membe 'kupasua jipu' la mgogoro Ziwa Nyasa



Na Rose Itono

WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Benard Membe, leo atazungumzia sababu za nchi ya Malawi kujiondoa katika mazungumzo ya mgogoro wa mpaka wa
Ziwa Nyasa na Tanzania.


Akizungumza Dar es Salaam jana, Bw. Membe alisema zipo
sababu ambazo atazieleza ili jamii iweze kuelewa na kufahamu
kwa nini nchi hiyo imeamua kufanya hivyo.

Hivi karibuni, Rais wa Malawi, Bi. Joyce Banda, alimuagiza
Waziri wake wa Mambo ya Nje kuvunja mazungumzo na
Tanzania baada ya nchi hiyo kutangaza rasmi uzinduzi
wa ramani mpya katika eneo la ziwa hilo.

Alisema Malawi imejiondoa katika mazungumzo ya ziwa hilo
na Tanzsania kutokana na kile anachodawi uchokozi, ubabe na vitisho vinavyofanywa na Tanzania dhidi ya raia wa nchi hiyo
na kusababisha mazungumzo ya utatuzi wa mgogoro huo
kuchukua muda mrefu.

Mgogoro huo umedumu muda mrefu tangu enzi za Rais wa Kwanza wa Tanzania, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Rais wa Kwanza wa Malawi, Hastings Kamuzu Banda.

Rais Banda alisema, nchi hiyo itaufikisha mgogoro huo katika mahakama ya kimataifa ili kutafuta muafaka badala ya kuendelea
na mazungumzo baina ya viongozi wa nchi hizo mbili.

Mvutano mkubwa uliopo ni kuhusu mpaka uliowekwa na
wakoloni walipoziga nchi hizo hasa mkataba unaofahamika
kama ‘Heligoland Treaty’ wa mwaka 1890.

Mkataba huo unaainisha mpaka kati ya Tanganyika na Malawi, haupiti katikati ya Ziwa Nyasa, bali ufukweni mwa ziwa hilo
hivyo kuifanya Tanzania kukosa miliki yoyote katika ziwa
husika ambalo limekuwa likitumiwa na wenyeji wa eneo hilo
upande wa Tanzania kwa muda mrefu.

Alisema ziwa hilo ambalo siku za karibuni limegunduliwa kuwa
na rasilimali kubwa ya mafuta na gesi, limezidisha mzozo baada
ya uongozi wa Malawi kuzipa zabuni kampuni zenye utaalamu wa gesi na mafuta kufanya utafiti na kuingia hadi eneo la Tanzania.

No comments:

Post a Comment