26 February 2013

CHADEMA wambana JK tatizo la udini



Na Elizabeth Joseph, Dodoma

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasi na Maendeleo (CHADEMA), ambaye pia ni Mbunge wa Mpanda Mjini, Bw. Said Arfi, ameitaka Serikali iwaeleze Watanzania kwanini inafumbia mambo tatizo la udini linaloendelea nchini.


Bw. Arfi aliyasema hayo mjini Dodoma jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Mwanga Bar, Kata ya
Uhuru na kusisitiza kuwa, tatizo hilo linaweza kuiweka nchi
mahali pabaya kwa siku za usoni.

Alisema Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali yake, bado haijachukua hatua zozote ili kuepusha machafuko yanayoweza
kutokea na kusababisha amani iliyopo kuwa historia.

“Awali Chama cha Wananchi CUF kilionekana cha Waislamu hivyo Wakristo wakakiogopa na kukimbia udini...hivi sasa CCM inadai CHADEMA ni chama cha Wakristo.

“Kutokana na propaganda hizi, tayari yameanza kutokea machafuko ambayo Wakristo na Waislamu wanapigana mapanga, tunamtaka Rais Kikwete alieleze Taifa kwanini chama chake kinasimamia
zaidi masuala ya udini,” alisema Bw. Arfi.


Aliongeza kuwa, baada ya mbinu za CCM kudai CHADEMA ni chama cha kikabila, sasa wameibuka na mbinu mpya wakidai
chama chao cha Wakristo jambo ambalio si kweli.

Alisema hivi sasa, CCM inatumia mamilioni ya fedha za wananchi katika mambo yasiyo na tija kwa jamii na Taifa badaya ya fedha hizo kuelekezwa katika sekta ya elimu ili kuongeza ufaulu wa
wanafunzi kwa lengo la kuongeza wataalamu.

“Tafiti mbalimbali zilizowahi kufanyika katika sekta ya elimu, zinasema uwekezaji mdogo katika sekta hii imechangia watoto wengi kuanza kidato cha kwanza wakiwa hawajui kusoma
wala kuandika lakini hakuna hatua zilizochukuliwa,” alisema.

Awali Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Mafunzo wa chama hicho Taifa, Bw. Benson Kigaila, aliwataka viongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, kujiuzulu kutokana na matokeo mabaya ya wanafunzi waliomaliza kidato cha nne mwaka 2012.

1 comment:

  1. Nadhani wamuulize KATIBA YA JAMUHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA INASEMAJE? maana ndio aliyoiapia na kuahidi kuwa atailinda na kuisimamia.Je anatekeleza? au imebadilika?

    ReplyDelete