05 February 2013

Aua watoto wake wawili, naye ajinyonga


Na Said Hauni, Lindi

MKAZI wa Kijiji cha Nakalonji, Kata ya Mbondo, Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi, Heseni Ng'ombe, amefariki dunia
baada ya kujinyonga kutokana na uliokuwa umejitokeza kati
yake na mkewe Bi. Sharifa Ally (26).

Kabla hajachukua uamuzi wa kujinyonga, marehemu aliwajeruhi kwa shoka watoto wake wawili Tunu Huseni (7) na Sheki Huseni (3), ambao wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya Nachingwea baada ya kukatwa sehemu mbalimbali za miili yao.

Habari zilizolifikia gazeti hili kutoka wilayani humo ambazo zimethibitishwa na Jeshi la Polisi mkoani humo, zimedai tukio
hilo limetokea Januari 28 mwaka huu, saa sita usiku.

Kamanda wa Polisi mkoani Lindi, George Mwakajinga, alisema
siku ya tukio, wanandoa hao walitofautiana ambapo mwanamke alidai talaka hivyo kuongeza hasira kwa mumewe (marehemu).

“Kutokana na hali hiyo, mwanaume alichukua shoka na kuanza kuwakata watoto wake na baada ya kuwajeruhi, marehemu alikimbilia msituni ambako alichukua kamba na kuamua
kujinyonga kwenye mti,” alisema Kamanda Mwakajinga.

Alisema majirani walimtafuta katika maeneo mbalimbali ya misitu ya kijiji hicho na kumkuta marehemu akining'inia juu ya mti akiwa tayari amefariki dunia.

“Marehemu baada ya kuwakata watoto wake kwa shoka, aliamini tayari wamekufa ndio maana na akaamua kujiua, baada ya wananchi kuiona maiti yake, walitoa taarifa polisi,” alisema.

Mganga wa zamu katika hospitali hiyo, Evelyne Mrumapili, alithibitisha kupokelewa watoto hao na kudai wamejeruhiwa
sehemu mbalimbali za miili yao hususan kichwani, mikononi.

“Hali ya Tunu aliyejeruhiwa mikononi inaendelea vizuri na Sheki aliyeumizwa kichwani hali yake ni mbaya amehamishiwa Hospitali ya Mission ya Ndanda iliyopo wilayani Masasi, mkoani Mtwara kwa ajili ya matibabu zaidi,” alisema Mrumapili.

No comments:

Post a Comment