05 February 2013

Wanawake washirikishwe katika shughuli za maendeleo



Na Christina Mokimirya

WITO umetolewa kwa jamii kuona umuhimu wa kuwashirikisha wanawake katika shughuli mbalimbali za maendeleo.

Ushauri huo umetolewa Dar es Salaam juzi na mshauri wa mambo ya utamaduni kutoka kitengo cha utamaduni cha Iran, Bw. Morteza Sabouri, wakati akitoa ujumbe katika maadhimisho kuzaliwa Mtume Muhamad (S.A.W) na Mapinduzi ya 34 ya Jamhuri ya Kiislamu nchini humo.

Alisema kila nyuma ya mwanaume aliyefanikiwa, kuna nguvu ya mwanamke iliyotumika hivyo ni bora wakashirikishwa katika mambo mbalimbali ili kuchochea maendeleo.

Aliongeza kuwa, katika kipindi cha mapinduzi nchini humo, mwanamke alitoa mchango mkubwa ili kuyafanikisha hivyo
ushiriki wa mwanamke katika masuala ya jamii, unaleta
maendeleo kwa jamii.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kislamu nchini (JUWAKITA), Shamim Khan, alisema Mtume Muhamad alianzisha amani na utulivu unaopaswa kuenziwa na kuwa njia ya maisha yetu.

Alzishauri familia kuishi kwa kuzingatia mafunzo ya Kiislamu
na maadili yake ili kupata maendeleo. Maadhimisho hayo yalishirikisha wageni kutoka nchini humo, viongozi
mbalimbali wa dini na Serikali.

No comments:

Post a Comment