19 February 2013

Amchinja mpenzi wake kinyama



Na Suleiman Abeid, Shinyanga

KATIKA hali isiyo ya kawaida, mkazi wa Kitongoji cha Shunu, mjini Kahama, mkoani Shinyanga, Bw. Mussa Petro (27), ambaye anafanya kazi ya kuchuna ngozi katika machinjio mjini humo, amemchinja mpenzi wake kwa kutenganisha kichwa na
kiwiliwili.


Kamanda wa Polisi wa mkoani humo, Evarist Mangalla, amesenma tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia juzi na kumtaja marehemu kuwa ni Jesca Elialinga (29), mkazi wa mji huo ambapo mauaji hayo yanahusishwa na wivu wa kimapenzi.

Alisema baada ya mtuhumiwa kufanya mauaji hayo, alichukua kisu alichotumia kumchinja marehemu na kujikata koromeo ili ajiue lakini hakufanikiwa mbali ya kupata jeraha kubwa shingoni.

Aliongeza kuwa, baada ya polisi kupata taarifa za mauaji hayo walifika eneo la tukio kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa ambaye alikimbizwa Hospitali ya Wilaya  ili kuokoa maisha yake ambapo hivi sasa anaendelea na matibabu hospitalini hapo chini ya ulinzi.

“Uchunguzi wa awali umebaini kuwa, chanzo cha mauaji haya ni wivu mapenzi...polisi wanaendelea na uchunguzi zaidi ili kubaini tatizo jingine kabla mtuhumiwa hajafikishwa mahakamani kujibu shtaka la mauaji baada ya kutoka hospitali,” alisema.

No comments:

Post a Comment