28 January 2013

Tunataka kutembelea miradi yote ya UKIMWI-Kamati ya Bunge



Na Rose Itono

WAJUMBE wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba,sheria na utawala wametaka kupewa umuhimu wa kutembelea mara kwa mara miradi na shughuli mbali mbali zinazohusiana na kampeni dhidi ya UKIMWI nchini ili kujua hasa thamani ya fedha zinazotolewa na serikali pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo katika kupambana na ugonjwa huo.


Wakiongozwa na mwenyekiti wao, Chana Pinda, wajumbe hao walitoa dai hilo jijini jana  walipokutana na viongozi wa ngazi za juu wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI (TACAIDS).

“Hatuwezi kuhakiki thamani ya fedha zinazoelekezwa katika miradi ya kupambana na UKIMWI kama tutaendelea kuletewa ripoti na taarifa kwenye makaratasi tu. Tunapaswa kufika kwenye maeneo ya miradi ili kuona walengwa wananufaikaje,” alisema Deogratius Ntukamazina, Mbunge wa Ngara na kiongozi mstaafu katika tume ya utumishi.

Kauli hiyo iliungwa mkono na Abbasi Mtemvu, Mbunge wa Temeke ambaye alisema ikiwa kamati itaendelea kutengwa katika shughuli muhimu zinazohusiana na kampeni dhidi ya UKIMWI, ni dhahiri itaendelea kupitisha bajeti ambayo huenda haiwanufashi walengwa.

Kama kamati haiwezi kufika huko kwenye miradi au halmashauri zinazopelekewa mamilioni ya pesa ili kupambana na UKIMWI kila mwaka, ni dhahiri kwamba kamati itakuwa inapitisha pesa ambazo haijui mwisho wa siku zinafanya nini, alisema Mtemvu
na kusisitiza umuhimu huo, mwenyekiti Chana Pinda alisema ziara kama hizo zitaiwezesha kamati yake kujua kinachoendelea huko kwenye jamii.

“Wajumbe wanataka ziara hizi sio kwa ajili ya posho, bali kwa ajili ya kutembelea miradi mbali mbali ya UKIMWI nchini na hivyo basi kuweza kujua kinachoendelea huko mashinani na kuchukua hatua stahiki,” alisema Pinda Wajumbe hao walitoa dai hilo mara baada ya naibu mwenyekiti wa TACAIDS Bi Beng’ Issa kutoa taarifa ya mwenendo wa kampeni dhidi ya UKIMWI nchini.

TACAIDS ndiyo mratibu wa shughuli zote a UKIMWI nchini ikifanya kazi chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu katika taarifa yake, alisema  kuwa licha ya kukabiliwa na ufinyu wa bajeti unaochangiwa na kupungua kwa misaada ya wahisani, serikali ilikuwa imejipanga kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI (VVU) kwenye jamii ya kitanzania kwa silimia 9 ili kufikia lengo hilo pamoja na mengine, serikali ilikuwa inajipanga kuhakikisha mfuko wa UKIMWI (AIDS Trust Fund) ambao ni jitihada za watanzania wenyewe unaanza kufanya kazi vizuri.

Takribani shilingi bilioni 300 zitakuwa zinakusanywa kutoka serikalini kupitia mfuko huo kila mwaka.

No comments:

Post a Comment