28 January 2013

CHANEDA kuandaa michuano maalumu



Na Mwali Ibrahim

CHAMA cha Netiboli Mkoa wa Dar es Salaam (CHANEDA), kukinatarajia kuandaa mashindano maalumu ya netiboli kwa timu za mkoa huo wiki ijayo, ili kuchagua timu ya mkoa.


Mashindano hayo yatafanyika katika Uwanja wa Bandari, Kurasini ambapo watachaguliwa wachezaji watakaounda timu hiyo, ambayo itashiriki michuano ya majiji yatakayofanyika Juni mwaka huu, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Msemaji wa CHANEDA, Michael Maurus alisema timu za Dar es Salaam zinatakiwa kujiandaa vyema ili kupata timu bora, itakayofanya vizuri katika michuano hiyo ya majiji.

"Tunataka Dar es Salaam ichukue ubingwa, licha ya sisi kuwa ndiyo waandaaji wa mashindano haya tunatarajia kuchagua wachezaji bora ili kuwa na timu bora ya jiji la Dar es Salaam na itakayokuwa bingwa kwa majiji mengine," alisema.

Ametoa wito kwa majiji mengine kujiandaa vyema, ili kuja kutoa upinzani katika mashindano hayo.

Majiji yatakayoshiriki michuano hiyo ni Mbeya, Mwanza, Arusha Tanga, Zanzibar na wenyeji Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment