15 January 2013

Adondoka kutoka juu ya Mnazi



Christina Mokimirya na Lead Daudi

MKAZI wa Mkuranga, mkoani Pwani, Mwarami Shamte (32), amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Kitengo cha Mifupa (MOI) baada ya kudondoka kutoka juu ya mnazi na kuumia sehemu mbalimbali za mwili wake.


Akizungumza na Majira Dar es Salaam jana, Ofisa Uhusiano wa MOI, Bw. Jumaa Almas, alisema Bw. Shamte alifikishwa hospitali hapo juzi jioni akitokea Mkuranga.

Alisema majeruhi huyo ameumia kichwani na sehemu nyingine
za mwili wakati akiangua nazi na hali yake bado haijaimarika.

Wakati huo huo, mwendesha pikipiki Bw. Elihuruma Nyaki, mkazi wa Kinondoni, Dar es Salaam, pamoja na abiria wawili wamelazwa hospitalini hapo baada ya kupata ajali katika maeneo tofauti.

Bw. Almas alisema Bw. Nyaki aligongwa na gari wakati akiwa na pikipiki na kujeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili wake ambapo abiria waliofikishwa hospitalini hapo ni Bw. Idd Ally (20), mkazi
wa Mbagala na Bw. Ramadhani Omary.

Alisema Bw. Ally amepata majeraha kwenye kichwa na sehemu mbalimbali za mwili wakati Bw. Omary amepata majeraha sehemu mbalimbali za mwili na wote wanaendelea na matibabu.


No comments:

Post a Comment