10 December 2012

Kikwete: Miaka 51 mafanikio ni mengi *Asema demokrasia ya vyama vingi imeimarika *Nape: Chama tawala kinastahili pongezi kubwa *Bi. Kidude, Ngurumo wapewa nishani za heshma





Rehema Maigala na David John

RAIS wa Jakaya Kikwete, jana alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara ambayo yalifanyika katika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam yakiwa na
kauli mbiu inayosema “Uwajibikaji, Uadilifu na Uzalendo ni nguzo ya Maendeleo ya Taifa letu”.

Viongozi wa nchi 12 za Kusini mwa Afrika (SADC), ambazo ni Namibia, Angola, Rwanda, Malawi, Zimbambwe, Mauritius, Msumbiji, Swaziland, Shelisheli, Losotho, Malawi, Congo (DRC), pamoja na nao walishiriki maadhimisho hayo.

Maadhimisho hayo pia yalihudhuriwa na Makamu wa Rais Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Rais mstaafu wa Awamu ya Pili, Alhaj Ali Hassan Mwinyi, Rais mstaafu wa Zanzibar, Aman Abeid Karume, mabalozi ambao wanaziwakilisha nchi zao nchini, viongozi wa vyama vya siasa, dini, wabunge, wanafunzi na wananchi.

Rais Kikwete aliwasili uwanjani hapo saa nne asubuhi akiwa katika gari la wazi pamoja na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama,
Jenerali Davis Mwamunyange na kutumia fursa hiyo kuwapungia mkono wananchi walioshiriki maadhimisho hayo.

Baada ya kushuka katika gari hilo, Rais Kikwete alipigiwa mizinga 21 isiyo na madhara kama ilivyotangazwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) pamoja na kukagua gwaride
ambalo liliandaliwa uwanjani hapo.

Wakati mizinga hiyo ikipigwa, watoto 10 wa halaiki walizimia kutokana na mshtuko wa mizinga hiyo wakati ikipigwa ambapo miongoni mwa askari wa Kikosi cha Wanamaji, naye alijikuta akiishiwa nguvu na kukaa chini baada ya kupigwa na jua kali.

Askari huyo pamoja na watoto wa halaiki ambao walianguka, walichukuliwa na wafanyakazi wa huduma ya kwanza na kwenda kupewa matibabu ya awali.

Gwaride lilipita mbele ya Rais Kikwete ambaye ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama kwa mwendo wa pole
na haraka pamoja na kutoa heshima ya utii.

Vijana wa halaiki nao walikuwa kivutio kikubwa kwa wageni waalikwa waliofika uwanjani hapo pamoja na vikundi mbalimbali vya ngoma za asili kikiwemo kikundi cha Taifa kutoka Rwanda.

Katika hotuba yake, Rais Kikwete alisema wakati Tanzania Bara ikiadhimisha miaka 51 ya uhuru, Taifa linajivunia mafanikio mengi, amani, utulivu na kukua kwa demokrasia ya vyama vingi vya siasa.

Alisema Tanzania imepata mafanikio ya utulivu wa kisiasa na kuwataka Watanzania kujipongeza wenyewe kutimiza miaka
51 kwa amani na utulivu.

Nape Nnauye

Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bw. Nape Nnauye, alisema wakati Taifa likiadhimisha
siku hiyo, Serikali inastahili pongezi kwa kuchochea maendeleo
katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu na miundombinu.

“Si kazi ndogo Taifa letu kufikisha miaka 51 ya uhuru wake bila kuwepo machafuko, wananchi wanaishi kwa amani na utulivu, hivi sasa nchi yetu inapiga hatua kubwa ya maendeleo,” alisema.

Bw. Nnauye alikiri kuwepo changamoto kubwa kwa baadhi ya Watanzania kuishi katika nyumba duni na kuwataka wanasiasa
wasijenge hoja ambazo hazina tija kwa Taifa bali washirikiane
na Serikali ili kuiwezesha nchi kufikia malengo yake.

James Mbatia

Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, Bw. James Mbatia alishauri wimbo ulioimbwa na vijana wa halaiki ambao unasema “tunafurahi kuzaliwa Tanzania”, ufundishwe katika shuleni zote nchini ili kuleta heshima na uzalendo kwa Taifa.

“Ndani ya miaka 51 ya uhuru wa Tanzania Bara, Watanzania asilimia 30 ni maskini hivyo changamoto kubwa iliyopo ni kuondokana na hali hii,” alisema.

Alisema ili kupunguza au kuondokana na umaskini uliopo, ipo haja ya kuongeza kasi ya kuwekeza kwenye elimu ambayo hivi sasa inaonekana kuwa dhaifu jambo ambalo ni hatari kwa nchi yetu.

Kutunuku nishani

Baada ya sherehe za maadhimisho ya miaka 51 ya uhuru, Rais Kikwete aliwatunuku nishani watu mbalimbali katika Viwanja
vya Ikulu, Dar es Salaam.

Waliotunukiwa nishani ya Jamhuri ya Muungano daraja la kwanza ni Balozi Ombeni Sefue na Dkt. Mohamed Seif Khatib. Nishani ya Jamuhuri ya Muungano daraja la pili ilitolewa kwa Jaji mstaafu Nicolous Munuo na Jaji Saimon Mkagununa.

Nishani ya utumishi mrefu na maadili mema daraja la kwanza ilitolewa kwa Alhaj Ramadhani Musa Kija, Bw. Peter Ananundura
na Bw. Ludovick Utouh. Nishani ya utumishi na maadili mema daraja la pili ilitolewa kwa Bw. Gabriel Maliseli na Ruth Rashidi

Waliotunukiwa nishani ya sanaa na michezo ni Fatuma Baraka Hamisi maarufu “Bi. Kidude”, Muhidini Maalim Ngulumo,
marehemu Marijani Rajabu, Fundi Said “Mzee Kipara”, na
John Steven Akwale

Utuzaji mazingira dalaja la kwanza Bw. Regnard Mengi na Dkt. Felistian kilahama. Nishani hiyo daraja la pili ilitolewa kwa
Valentini Msusa. Nishani ya Mwenge wa Uhuru dalaja la nne ilitolewa kwa Kamishina Jenerali wa Magereza John Minja,
Said Kamtawa (aliyekuwa dereva wa kwanza wa hayati
Mwalimu Julius Nyerere).

Wengine ni Samwel Sandai (alishiriki kupinga ukoloni), Ndete Athumani, Juma Nkumba na Kingdom Koloso. Nishani ya
Ugunduzi na Utafiti wa Kisayanzi ilitolewa kwa Dkt. Joseph Nduguru, Dkt. Geoge Nngode, Dkt. Catherini Madata na Dkt.
Alfred Mosha

Nishani ya ushupavu ilitolewa kwa MT 8183 Meja Hassani, PF 15 Mohamed Kilonzo, MT 7748 Privete Kongo Hamed Basha, MT 9023 Privete Deus Hamisi Lugela, MT 87245 Private Yafeti Gama,
MT 97213 Privete Ali Simba, MT 97209 Privete Alli Juma Hamed,
MT 79959 Koplo Emanuel Komalo, MT 83865 Privete Juma Dadi
na XG 5428 T.S Kumaija.

3 comments:

  1. He vipi Mbaraka Mwinshehe, Juma Kilaza, Patrick Balisidya, Mzee Jongo, Hamisi Tajiri, Mama Haambiliki, n.k ? Raisi amesahau kulikuwa na kina Sembuli, Chogo, Kajole, Masimenti, Mahadhi, Gobos, Jela Mtagwa, n.k.? Hivi kweli Bi Kidude ni mfano mzuri kwa jamii? Usiangalie uzee wake angalia maadili yake toka usichana, kuna mzazi mwema atakayependa bintiye aige tabia za Bi Kidude? Au kwa kuwa wazungu wanamsifia? Kweli hizi nishani sasa anaweza kupata yeyote! Enzi za mzee wa Butiama haikuwa rahisi hivi! Hebu fikiria unapewa nishani katika sherehe moja na mama anayjidai kwa kubadili wanaume toka udogo wake! Mwe!

    ReplyDelete
  2. Kutokana na changamoto zilizopo za kuwapata watu sahihi wa kupewa Nishani, ni vizuri sasa Serikali ikaweka utaratibu maalum wa kuwapata watakaotunukiwa nishani. Utaratibu huo unapaswa kuwa shirikishi na ukiangalia sekta kwa sekta. Aidha, utaratibu huo uanzie kwenye ngazi ya wilaya, mkoa na Taifa. Vigezo muhimu vya kuwapata watakaopewa nishani hizo viwekwe wazi, vinginevyo nishani hizo zinaweza kupoteza maana halisi iliyokusudiwa.Watakaopewa nishani hizo ionekane kweli wanastahili pasipo shaka.

    ReplyDelete
  3. JE NI KELI ASIYE NA MACHO HAAMBIWI TAZAMA?NUKUU YA JUMAPILI TOKA UWANJA WA TAIFA 1. SERIKALI IWAWAJIBISHE ASKARI WANAOTISHIA WAANDISHI WA HABARI

    ReplyDelete