21 November 2012

Mauaji mtoto wa Fundikira hukumu yake kutolewa leo



Na Rehema Mohamed

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, leo inatarajiwa kutoa hukumu ya akesi ya mtoto wa marehemu Chifu Abdallah Fundikira,  inayowakabili MT 1900 Sajenti Roda Robert (42) wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Kikosi cha Mbweni na wenzake.

Hukumu hiyo inatarajiwa kutolewa mbele ya Jaji Zainabu Mruke, ambapo washtakiwa wengine ni MT 75854 Koplo Ally Ngumbe (37) wa Jeshi la Ulinzi la  Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Kikosi cha Kunduchi na MT 85067 Koplo Mohamed Rashid wa JKT Mbweni.

Katika kesi hiyo, inadaiwa kuwa Januari 23,2010, saa sita usiku 6 usiku marehemu Swetu Fundikila, akiwa na wenzake wawili katika gari aina ya Toyota Corolla, wakitokea Mwananyamala walikutana na washtakiwa hao eneo la Kinondoni wakiwa kwenye gari lao wakitokea kwenye maegesho ya magari Baa ya Mango Garden.

Ilidaiwa kuwa, mshtakiwa wa kwanza (MT 1900 Sajenti Roda Robert), alimwamuru dereva wa gari ambalo ndani alikuwepo marehemu, arudi nyuma na dereva huyo kutii amri hiyo.

Washtakiwa hao walilifuata gari hilo na kusimama pembeni ambapo mshtakiwa MT 1900 Sajenti Robert alishuka kumfuata dereva na kumuonya kuwa siku nyingine asipowaheshimu viongozi wa nchi atapata shida.

Baada ya hapo marehemu na wenzake waliondoka lakini walipofika katika makutano ya Barabara ya Kawawa,  walikutana tena na washtakiwa ambapo MT 1900 Sajenti Robert akawatukana.

Inadaiwa marehemu aliuliza sababu ya kuwatukana bila kosa, lakini badala yake MT 1900 Sajenti Robert aliaanza kumpiga dereva wa gari lao na kumfanya marehemu kwenda kumsaidia asipigwe.

Kitendo hicho kilisababisha ugomvi huo kuamia kwa marehemu ndipo washtakiwa walimchukua kwa madai ya kumpeleka Kituo
cha Polisi lakini hakupelekwa huko na badala yake aliokotwa
kwenye fukwe za Upanga akiwa hoi kwa kipigo na baadaye
alifariki dunia akiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

No comments:

Post a Comment