19 November 2012

MAPADRI WA ITALI WATISHIA KUKIMBIA.Ni baada ya kujeruhiwa na majambazi

Na Eliasa Ally, Iringa
November 17, 2012

Mapadre wa Misionari wa kutoka Nchini Italia wanaofanya kazi za kanisa mkoani Iringa
wametishia kuondoka baada ya padre mwenzao Angelo Burgio wa Italia kupigwa risasi na
kuporwa fedha katika parokia ya Lwang'a ambapo wamesema kuwa hali ilivyo kwa sasa ya
usalama kwa watumishi hao wa Kanisa ni mdogo na wametaka misaada yote
wanayoifadhilia kwa wananchi na waumini maeneo ya vijijini wataacha kuendelea
kufadhili.

Wakizungumza na Majira leo wakati wakimtembelea Padre Angelo Burgio Hospitali ya
Mkoa wa Iringa, baadhi ya mapadre hao walisema kuwa kwa sasa hali ilivyo nchini
Tanzania siyo ya amani na kuonge kitendo cha kuvamiwa misheni za Kanisa Katoliki
kinawatia hofu na kuondoa imani ya kuendelea kufanya kazi kwa amani.

Akizungumzia hali hiyo, Padre Salvatory wa Parokia ya Idodi alisema kuwa
 wanashangazwa na kuvamiwa kwa Padre Angelo ambaye amekaa nchini Tanzania zaidi ya
miaka 30 huku akifanya shughuli mbalimbali za maendeleo ya kijamii kwa wananchi na
waumini wengine na kusema kuwa hiyo ni dalili tosha ambayo inaonesha watanzania
hawataki misaada ambayo inatolewa na wamisionari hao ya maji, vituo vya afya, kulea
watoto yatima na kuwasomesha wengine katika ngazi zote za elimu.

Waliongeza kuwa kwa sasa wanawasiliana na ubalozi wao nchini Tanzania ili kuweza
kueleza hali halisi na kusitisha kuendelea kutoa huduma mbalimbali kwa waumini na
wananchi kutokana na hali ya kiusalama kuwa kwa sasa inatishia na kuongeza kuwa
vitendo vya uvamizi vimewatia hofu kubwa sana wao kwa kuwa hawajawahi kufanyiwa vitu
kama hivyo na walikuwa wanategemea kuwa jamii ya watanzania ni watu wema.

Wamesema kuwa huduma zao wanazitoa katika maeneo ya vijijini ambako hakuna hata
vituo vya polisi na kuongeza kuwa kutokana na hali ya kuvamiwa ilivyo sasa
 inawatia hofu kwa kuwa maisha yao yanaweza kuendelea kuwa hatarini na kuweza
kuvamiwa na majambazi hali ambayo inawatia mashaka kwa kuvamiwa makanisa bila
kumwogopa hata Mungu.



No comments:

Post a Comment