20 September 2012

Mufti,Shekhe Ponda waungana kulaani kudhalilishwa uislamu


 Stella Aroan na Salim Nyomolelo

BARAZA Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) limelaani vikali filamu ya Innocence inayodaiwa kumdhalilisha Mtume Mohammad (S.A.W) na limeitaka Marekani kuwachukulia hatua waliohusika.

Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya BAKWATA, Dar es Salaam jana Mufti Mkuu wa Tanzania Shekhe Issa bin Shabaan Simba, alisema filamu hiyo licha ya kumtukana na kumdhalilisha Mtume Mohammad, lakini pia inachochea uhasama na chuki baina ya wafuasi wa dini mbalimbali.

"BAKWATA na Waislamu kwa ujumla tumesikitishwa na kuhuzunishwa na filamu hii ambayo lengo lake ni kuchafua heshima na thamani aliyonayo kiongozi wetu  (Mtume Mohammad) na kudhalilisha uislamu kwa makusudi," alisema Sheikh Simba

Alisema kitendo cha watu kuwa na uhuru wa kufanya wanavyotaka kwa kisingizio cha demokrasia na uhuru wa haki za binadamu ndiyo chanzo kikubwa cha kuibua hasira za waislam ulimwenguni kote na kusababisha watu wasiokuwa na hatia kupoteza maisha.

Alisema kuwa wanaitaka Serikali ya Marekani kuipitia upya sheria yake ya uhuru wa kueneza habari ili kuwe na namna ya kuzuia kuwakashfu viongozi wakuu wa dini pamoja na kuyagusa au kuyakejeli mambo yanayohusu uislamu.

Sheikh Simba alisema mara nyingine hali hiyo inaweza kusababisha vita vya kiimani kama kila upande utapinga kutukanwa na kudhalilishiwa viongozi wao wakuu wa dini, jambo ambalo wasingependa litokee mahali popote duniani.

Alisema kuwa licha ya Waziri wake wa Mambo ya Nje wa Nchi, Bi. Hilary Clinton, kukanusha suala hilo ni vyema wahusika wakachukuliwa hatua stahiki na mambo hayo yasitokee tena nchini humo.

Alisema kuwa wanaitaka serikali ya nchi hiyo kupiga marufuku filamu hiyo, ikiwa ni pamoja na kuzilazimisha kampuni zenye kuendesha mitandao mbalimbali kuiondoa filamu hiyo pamoja na kumchukulia hatua kali mtayarishaji wa filamu hiyo.

Wakati huo huo, waislamu wanatarajia kufanya mkutano mkubwa jijini
Dar es Salaam kesho, kulaani filamu hiyo na kutoa matamkoa mbalimbali, likiwemo la kususia bidhaa zinazozalishwa Israel na Marekani.

Mkutano huo unaoratibiwa na jumuiya za taasisi za kiislamu, unatarajiwa kufanyika  Viwanja vya Jangwani.

Akizungumza na gazeti hili jana Katibu Mkuu wa Jumuiya na Tasisi za
Kiislamu Tanzania, Shekhe Ponda Issa Ponda, alisema wamefikia
hatua hiyo kutokana na udhalilishaji mkubwa uliofanywa kwenye filamu hiyo.

Kwa mujibu wa katibu mkuu huyo mtunzi wa filamu hiyo ameonesha
udhalilishaji mkubwa kwa kiongozi wao wa dini na waumini wake kwa
ujumla.

"Hatuwezi kunyamazia kimya kitendo hiki kwani si cha kudhalilishwa
kwa waislamu tu bali watu wote kwani ni kibaya na kinaweza
kuchochea masuala mengine," alisema.

Shekhe Ponda alisema katika mkutano huo unaoratajiwa kufanyika
kesho kutakuwa na matamko mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwaeleza
waislamu kususia bidhaa zote zinazozalisha na mataifa ya Israel na
Marekani.

Alisema kutakuwa na mabango yenye ujumbe wa aina mbalimbali wa
kulaani filamu hiyo, hivyo amewataka waislamu wote bila ya kujali
tofauti zao kuhudhuria mkutano huo.

"Mkutano huu ni kwa ajili ya waislamu wote hata wasio waislamu,
kwani kitendo hicho ni cha udhalilishaji na kibaya kwa kiongozi
mkuu wa dini," alisema Shekhe Ponda.


Filamu hiyo iliyotengenezwa na Mmarekani mwenye asili ya Israel,
Sam Bacile (52) ilitengenezwa California nchini
Marekani ikiwashirikisha wasanii mbalimbali.

Filamu hiyo inayodaiwa kuwadhalilisha waislamu inaigizwa kwa  lugha ya kiingereza ikiwa na tafsiri ya  maandishi kwa kiarabu.
Filamu hiyo imegharimu dola za Marekani milioni tano kuitengeneza
kwa msaada wa mayahudi 100 waliojitolea kuchangishana fedha za
kuitengeneza filamu hiyo

No comments:

Post a Comment