24 August 2012

Mishahara ya walinzi sekta binafsi yapanda



Jesca Kileo na Darlin Said

CHAMA cha Sekta ya Ulinzi Binafsi nchini (TSIA), kimetangaza viwango vipya vya mishahara ya walinzi wa kampuni binafsi ambayo imepanda kwa zaidi ya asilimia 100.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa TSIA, Bw. Almas Maige, alisema chama hicho kimetoa viwango elekezi ili viweze kutumiwa na waajiri kuwalipa mshahara walinzi wao.

Alisema uamuzi huo umefikiwa baada ya kugundua kuwa, ghamara zilizokuwa zikilipwa na wamiliki wa kampuni kwa mlinzi mmoja mmoja ukilinganisha na pesa wanazotoa wateja ni kidogo.

“uanzia sasa kiwango cha chini cha mlinzi atakayekuwa lindo na silaha ni sh. 210,000 badala sh. 80,000 za awali, posho ya saa za ziada itakuwa sh. 50,000,” alisema.

Bw. Maige aliongeza kuwa, Agosti 14 mwaka huu, Wakala wa Manunuzi Serikalini (GPSA) kwa kutumia Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Manunuzi ya Umma (PPRA), ilitangaza zabuni ya kazi za ulinzi na gharama elekezi za shughuli hizo kwa mlinzi mmoja.

Aliongeza kuwa, gharama hizo hazikuendana na gharama halisi za mlinzi mmoja mmoja ambapo TSIA iliwasilisha mapendekezo yake kwa kigezo cha mshahara wa sh. 80,000 na marupurupu mengine.

Bw. Maige alisema mbali na mshahara kuwa sh. 80,000, pia  walipendekeza walipwe posho ya saa za ziada sh. 63,999, fedha za likizo sh. 6,666 kwa mwezi, makato ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii asilimia 10, sawa na sh. 14,399, na marupurupu mengine yanayofanya mashahara wa mlinzi kufikia sh. 210,000.

Alisema baada ya kuwasilisha mapendekezo hayo, Serikali iliridhia mshahara kwa mlinzi kutoka sh. 80,000 hadi 210,000 na kuwataka wamiliki wa kampuni hizo, kuanza kuwalipa mshahara huo wafanyakazi wao mara moja.

No comments:

Post a Comment