28 August 2012

ADC kupata cheti usajili wa kudumu



Na Rehema Maigala

CHAMA Kipya cha Siasa nchini, Alliance for Democratic Change (ADC), leo kinatarajia kupata cheti cha usajili wa kudumu baada ya kumaliza uhakiki wa wanachama katika mikoa 10 ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa chama hicho, Bw. Saidi Miraji, alisema cheti hicho kitatolewa na Msajili wa Vyama vya Siasa nchini Bw. John Tendwa.

“Tumetimiza vigezo vinavyotuwezesha kupata usajili huu kisheria ili tuweze kuingia katika kinyang'anyoro cha kampeni za uchaguzi mdogo Jimbo la Bububu, Zanzibar kwa kusimamisha mgombea.

“Uchaguzi mdogo katika jimbo hili unatokana na kifo cha aliyekuwa mwakilishi wake, marehemu Salumu Amir Mtondoo,” alisema.

Aliongeza kuwa, baada ya kupokea cheti hicho watakuwa na Mkutano Mkuu wa Taifa ambao utahudhuriwa na wanachama zaidi ya 200 kutoka mikoa mbalimbali nchini.

Alisema katika mkutano huo, kutakuwa na agenda tatu muhimu ambazo zitazungumzwa ikiwemo kupokea taarifa za kazi za chama kwa kipindi chote tangu kianzishwe, kupitisha ya katiba na kuwathibitisha viongozi wao.

No comments:

Post a Comment