06 July 2012

Wapenzi wateketea kwa moto chumbani *Walikuwa wamelala usiku, chanzo cha moto 'utata'


Na Waandishi Wetu

WATU wawili ambao ni mtu na mpenzi wake, wamefariki dunia baada ya kuteketea kwa moto katika nyumba waliyokuwa wamelala.

Akizungumza na gazeti hili, mjumbe wa shina namba 48. eneo la Keko Toroli, Bi. Zubeda Sobo, alisema tukio lilitokea usiku wa manene baada ya moto kuzuka ghafla katika chumba hicho.

“Juhudi za kuwaokoa na kuzima moto zilishindikana, pembeni mwa nyumba waliyokuwa wakiishi kuna kisima cha maji ambayo tulichota kuzima moto huu lakini tukakuta wote wameshaungua,” alisema Bi. Sobo.

Alisema marehemu hao wanafahamika mtaani kwani ni marafiki wa muda mrefu ambapo msichana huyo, humtembelea rafiki yake na kulala mar kwa mara.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Temeke, David Missime, alisema tukio hilo lilitokea jana saa 8.30 usiku.

Alimtaja mwanaume aliyekufa ni Bw. Yusuf Madi (20) ambaye ni fundi seremala na mwanamke Bi. Pendo Ndetaulo, ambapo nyumba hiyo ina vyumba vitatu.


“Chanzo cha moto huu bado hakijafahamika ila inahisiwa ni mshumaa ambao labda walikuwa wameuwasha kabla ya kulala,” alisema Kamanda Missime.

No comments:

Post a Comment