05 July 2012

Wafanyakazi Barclays wadaiwa kuiba dola za Marekani 34,000


Na Rehema Mohamed

WAFANYAKAZI wawili wa Benki ya Barclays na mfanyabiashara mmoja, jana wamepandishwa kortini katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, kwa kosa la kula njama na kuiba dola za Marekani 34,000.

Washtakiwa hao ni Bw. Wilscate Ushiwe (20), Bw. Ramadhani Wagole (35) na mfanyabiahara Bw. Desire Mangongo (39).

Mbele ya Hakimu Bw. Faisal Kahamba, wakili wa Serikali Bi. Willa Haoga, alidai katika tarehe zisizofahamika mwaka huu jijini Dar es Salaam, washtakiwa walikula njama ya kutenda makosa hayo.

Katika kosa la kwanza, ilidaiwa Januari 14 mwaka huu wakiwa katika benki hiyo iliyopo eneo la Slipway Msasani, wilayani  Kinondoni, washtakiwa waliiba dola za Marekani 9,000 kutoka akaunti namba 0127000379 ya Bw. Mohamed Salehe.

Shtaka la pili, inadaiwa Januari 20 mwaka huu, washtakiwa waliiba dola za Marekani 12,000 kutoka akaunti namba 0127020379 ya Bw. Mohamed Salehe.

Katika shtaka la tatu, inadaiwa Januari 25 mwaka huu, washtakiwa waliiba dola za Marekani 13,000 kutoka akaunti namba 0127020379 ya Bw. Mohamed Salehe.

Washtakiwa wote walikana kutenda makosa hayo ambapo upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi haujakamilika.

Hakimu Bw. Kahamba alidai washtakiwa wanaweza kuwa nje kwa dhamana kama watatimiza masharti ya kuwa na wadhamini wawili ambao watasaini hati ya dhamana ya sh. milioni 10 kila mmoja.

Vigezo vingine ni kila mshtakiwa kuwasilisha mahakamani sh. milioni 10 taslimu au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani hiyo. Washtakiwa wote walishindwa kutimiza masharti hayo na kurudishwa rumande. Kesi imehairishwa hadi Julai 18 mwaka huu.


No comments:

Post a Comment