05 July 2012

Serikali: Hakuna uthari za kiafya maji yenye tindikali North Mara



Na Benedict Kaguo, Dodoma

SERIKALI imesema hakuna ushahidi wowote wa kisayansi ambao unaonesha athari za kiafya zilizojitokeza kwa baadhi ya waathirika wa tukio la kumwagika tindikali kwenye mabwawa katika mgodi wa dhahabu wa North Mara.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Muungano, Bi. Samia Suluhu Hassan, aliyasema hayo bungeni mjini Dodoma jana wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2012/13.

Alisema matatizo ya kiafya na vifo vinavyodaiwa kutokea katika mgodi wa North Mara kutokana na uharibifu wa mazingira, Serikali iliahidi kutoa taarifa.

Aliongeza kuwa, Serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, ulichukua sampuli za maji yaliyokuwa kwenye visima mbalimbali vinavyozunguka mgodi huo na nje ya mgodi wa Nyamongo.

“Sampuli hizi zilionesha kulikuwa na viwango vya juu vya madini tembo (heavy metals), uchunguzi wa sampuli za damu ambazo  zilizochukuliwa kutoka kwa baadhi ya wakazi wa vijiji ambavyo vinazunguka mgodi na mifugo.

Alisema kutokana na kugundulika kwa kiwango hicho cha madini katika vyanzo vingi vya maji eneo la Nyamongo, Wizara ya Maji kwa kushirikiana na uongozi wa mgodi, walifanya jitihada za haraka kupata vyanzo vya maji mbadala kwa matumizi yao.

Baada ya hapo, Wizara kwa kushirikiana na mgodi huo, walichimba visima vya maji ambayo yameonesha kuwa na kiwango kidogo cha madini hayo.

Matumizi ya mifuko ya plastiki

Alisema mwaka wa fedha 2011/12, ofisi hiyo iliendelea kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa agizo la Serikali la kupiga marufuku uingizaji, utengenezaji, uuzaji na matumizi ya mifuko ya plastiki yenye unene chini ya mikroni 30, iliyoanza kutumika Oktoba 2006.

Alisema kutokana na changamoto zilizojitokeza katika kutekeleza kanuni za mwaka 2006 ambazo zinapiga marufuku matumizi hayo, Serikali iliahidi kuchukua hatua ya kupiga marufuku matumizi ya mifuko laini ya plastiki ili kulinda mazingira na afya ya binadamu.

Aliongeza kuwa, ili kutekeleza azma hiyo walishirikiana na wadau wengine kupitia kanuni za zamani na kuandaa kanuni mpya kuhusu matumizi ya mifuko laini ya plastiki.

“Kanuni mpya zimetoa fursa ya kutumika kwa baadhi ya bidhaa za plastiki kwa ajili ya shughuli muhimu kwenye viwanda mbalimbali  ikiwemo sekta ya maziwa na usindikaji vyakula,” alisema.

No comments:

Post a Comment