15 December 2011

Mrema: Posho zitatugombanisha na wananchi

*Amshangaa Rais Kikwete kumnyima nishani

 Na Gift Mongi, Moshi

CHAMA cha Tanzania Labour Party (TLP), kimesema nyongeza ya posho za wabunge kutoka sh. 70,000 hadi sh.200,000, haiendani na hali halisi ya uchumi wa Mtanzania hivyo kama zitatolewa,
zitamchonganisha mbunge na wananchi waliomchagua.

Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Bw.Augustino Mrema, aliyasema hayo mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema msimamo wa chama hicho ni kupinga nyongeza hiyo kwani Watanzania wanakabiliwa na changamoto nyingi hivyo ni bora fedha hizo zikatumika kuharakisha maendeleo ya sekta mbalimbali.

Bw. Mremba ambaye pia ni Mbunge wa Vunjo, alisema wazo la kuongeza posho za wabunge limetolewa kwa kukurupuka bila kuangalia madhara yanayoweza kumpata mbunge husika.

“Mtu aliyetoa wazo hili amekurupuka, fedha hizi ni nyingi sana bora ingekuwa sh. 100,000, kimsingi nchi yetu ina matatizo mengi, baadhi ya watumishi serikalini wanalipwa mishahara midogo hivyo fedha hizi wangeongezwa wao pamoja na walimu,” alisema.

Katika hatua nyingine, Bw. Mrema amesema nishani zilizotolewa na Rais Jakaya Kikwete kwa baadhi ya viongozi kama ishara ya kutambua mchango wao katika kilele cha maadhimisho ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania bara ni unafiki mtupu.

“Hadi sasa sijui Rais Kikwete ametumia vigezo gani kutoa nishani hizi, baadhi ya viongozi waliopewa bado hawajamalizia muda wao wa utumishi serikalini na mchango wao hauonekani.

“Inashangaza kuona kiongozi amedumu katika nafasi hiyo mwaka mmoja tu lakini anapewa nishani kwa mchango upi?...miaka ijayo akiharibu itakuwaje kama sio unafiki hivyo ni bora hizi nishani zikapigiwa kura na wananchi,” alisema Bw. Mrema.

Aliongeza kuwa, wapo baadhi ya viongozi ambao mchango wao unaonekana katika jamii lakini hawakupewa nishani hizo akiwemo yeye mwenyewe ambaye aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali serikalini, Waziri wa Afrika Mashariki, Bw.Samuel Sitta na Waziri Mkuu mstaafu, Bw. John Malecela.

“Mheshimiwa Spika Bi. Anne Makinda hana muda mrefu katika uongozi lakini kapewa nishani, hii inashangaza sana ni bora wananchi wapewe nafasi ya kupiga kura ili kuchagua viongozi wanaostahili kupewa heshima hii,” alisema.

Alisema hata kama Rais Kikwete ameshindwa kumpa nishani kutokana na mchango wake kwa Taifa hili, hakuwa na sababu ya kuwanyima viongozi wengine ili kuondoa dhana kuwa, nishani hizo zimetolewa kwa kujuana.

Wakati huo huo, Mwandishi Pamela Mollel, kutoka Arusha anaripoti kuwa, baadhi ya wasomi, wanaharakati na viongozi wa dini nao wametangaza msimamo wa kupinga nyongeza ya posho za wabunge na kudai kuwa, gharama za maisha hazijapanda kwa Mkoa wa Dodoma pekee bali katika mikoa yote nchini.

Wakizungumza na Majira kwa nyakati tofauti, walisema nyongeza hiyo imelenga kuboresha maisha ya wabunge badala ya kuangalia hali halisi ya maisha ya Watanzania.

Walisema makundi mbalimbali yamekuwa yakiishi katika maisha magumu hususan askari polisi, magereza, watumishi wa sekta ya afya pamoja na walimu.

Katibu Mtendaji wa Mtandao wa Mashirika yasiyo ya
kiserikali mkoani Arusha (Angonet,) Bw. Peter Bayo, alisema ongezeko hilo haliwezekani kwani utetezi wa Spika wa Bunge, Bi. Anne Makinda kuwa gharama za maisha zimepanda mjini Dodoma, hauna tija kwani gharama hizo zimepanda nchi nzima.

“Ongezeko hili linapaswa kutazamwa kwa mapana hasa kwa kuangalia uhalisia wa maisha ya Mtanzania badala ya kuangalia kundi moja la wabunge pekee.

“Bunge lina wajibu wa kutazama hali ya maisha ya Watanzania wote na kuporomoka kwa shilingi badala ya kuangalia maisha yao,” alisema Bw. Bayo.

Kwa upande wake, Mchungaji wa Kanisa la Blessing Alter, liliopo Sanawari, Isaya Sizya, alisema haoni tatizo la nyongeza hizo lakini ongezeko hilo ni linapaswa kuwagusa na watumishi wa idara
mbalimbali serikalini.

Alisema ni vyema Bunge likawa na sababu za msingi juu ya ongezeko hilo kwani katika jamii kuna makundi muhimu kama watumishi wa sekta ya afya, walimu na askari ambao nao wanastahili nyongeza ya posho za kujikimu.

“Mimi napendekeza ongezeko la posho za vikao vyao iendelee kubaki sh. 70,000 au sh. 100,000 kwani sh. 200,000 ni nyingi sana ukilinganisha na makundi mengine ya watumishi ndani ya jamii.

“Sio kwamba tunawaonea wivu wabunge wetu ila kuna makundi muhimu ya watumishi ambayo yanapokea posho kiduchu,” alisema.

Mkuu wa Kitivo cha Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Makumira, kilichopo nje kidogo ya Jiji la Arusha, Elfuraha Laltaika, alipinga ongezeko hilo na kudai kuwa, sababu zilizotolewa na Bi. Makinda hazina tija.

Alisema wapiga kura wamechagua wawakilishi wa kwenda kuwasemea sio kuongezeana posho za vikao badala ya kuyatizama makundi mbalimbali ndani ya jamii.

“Huu ni ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma kama ulivyo unadhirifu mwingine, wabunge wametuangusha sisi tuliowachagua wakatutetee badala yake wanataka kuongezeana posho,” alisema.

14 comments:

  1. Wabunge wetu wameonyesha udhaifu mkubwa sana na kutokuwajibika kwa jamii ya Watanzania waliowachagua. Huo ni usaliti mkubwa na wameonyesha udhaifu katika kutimiza majukumu waliyoaminiwa na wananchi. Walitakiwa kuangalia kwa upana hali ya maisha ya watanzania wote na sio kujifikiria wao peke yao. Hii inatia mashaka sana kama wabunge wetu kweli wanatetea maendeleo ya wananchi wote au wanaangalia maslahi yao binafsi. Nawashauri wakumbuke walikotoka na ahadi zao wakati wa kuomba kuchaguliwa. Nafurahi kwamba CCM na vyama vingine vya siasa vimekataa hoja hiyo. Na wewe Spika (Makinda) acha ubinafsi, badili msimamao wako usionekane msaliti wa watu wako wa Njombe. Laki mbili kwa posho ya siku moja wakati watumishi wengine wa umma hata mshahara wa mwezi haufiki hapo! Hiyo ni dhambi kubwa mbele za Mungu.

    ReplyDelete
  2. It is unbelievable how our Honourable Wabunge behave! How can they be so selfish? No wonder why during election campaigns they struggle so much to go to mjengoni in the pretext that they are going for the sake of wananchi's development while in the actual fact they are going to fill their never satisfied big bellies. Please stop this act. My appeal to the President is "please don't approve this proposal"

    ReplyDelete
  3. Kwa kweli ongezeko hili la posho kwa wabunge tu lifutwe. Maisha yamepanda sana kwa wananchi wote wa Tanzania iweje wabunge tu ndio watizamwe. Huyu Mama Makinda nishani aliyopewa ni ya kusimama kidete kuhakikisha maslahi ya wakubwa yanalindwa na si vinginevyo. Uspika wa Bunge ana mwaka mmoja tu anapewa nishani siku akiharibu atanyang'anywa? Miaka iliyobaki minne ndio mingi kuliko aliyotumika Bungeni. Au anapongezwa kwa ubabe anaoutumia bungeni? Mh. Rais kama kuna udhaifu ameshauonyesha huu ndio umetia fora. TZ hatuna viongozi kwani uongozi uliopo ni wa kishikaji na sio kiutendaji.

    ReplyDelete
  4. Kama mambo yenyewe ni hayo (kujazana mapesa kwa wingi), basi ubunge uwe wa mgawo kama umeme. Mtu akipata iwe ni mara moja tu kisha aachie wengine ili nasi wengine tufaidi. Ndio maana naona hawa jamaa siku zote ni kujipendelea tu, posho, mishahara na mengine mengi tusiyoyajua ilimradi tu wapate pesa. Ah Tumechoka kusiki ya posho badala ya masuala ya maendeleo

    ReplyDelete
  5. Watanzania Tuache kuwalalamikia wabunge. Tujipange kuikomboa nchi yetu hapo 2015. CCM Down

    ReplyDelete
  6. wakati nchi haina maji ya kutosha, hospitali za serikali duni, elimu mashuleni imeshuka, wanafunzi hawana vitendea kazi , walimu hawana mishahara ya kutosha, wabunge vipi wanataka posho zaidi ikiwa wau kweli waliingia kwenye siasa kwa ajili ya kuhudumia wananchi ilitakiwa wawe mfano kwa kuchukua mapato madogo bila ya kutaka ziada , lakini kwa bahati mbaya siasa zetu hapa ni mradi wa kujitajirisha. Wananchi tuamke hakuna cha CCM wala CHADEMA wala CUF wote wanataka maslahi , hao CHAdema na CUF wakipata serikali haitakuwa chochote , watatusahau. Wananchi tuamke tuandamane kushinikiza serikali kurejea mapato na mishahara ya fani zote , wanasiasa , mawaziri , wabunge, viongozi wa serikali, polisi , jeshi wawe ni watu wa mishahara ya chini kabisa kwa sababu wao wanasema wana uchungu na raia basi wawe mstari wa mbele na mfano kwa raia kujitoa mhanga kwa hilo.

    ReplyDelete
  7. Hawa wabunge ni hatari kubwa, lakini hivyo ndivyo ilivyo serikali yetu(wabunge wengi wa CCM).

    Lakini pamoja na kelele zote hizi utashangaa imeidhinishwa na tutabaki midomo wazi. CCM DOWN immediately!!

    ReplyDelete
  8. UCHUMI unatumikia SIASA badala ya SIASA kutumikia UCHUMI. Hivyo wananchi wasitegemee maendeleo yoyote ya maana ya kuwanufaisha wao, bali wanasiasa wataendelea kunufaika kwa sana. WATAALAMU wanaacha nafasi walizozisomea na kugombea nafasi za kisiasa ili wapate kipato kikubwa kwa kudanganya na kusema yasiyowezekana na ambayo hawakuyosomea. Sehemu za uzalishaji kama viwandani, mashuleni, vyuoni,n.k zinakosa watendaji kila mtu anataka kuwa Mbunge, Diwani n.k Je tutafika? HAIWEZEKANI

    ReplyDelete
  9. Mimi ninachofikiri, hizi posho, zilikuwa Indirect bribes especial to CCM,members for passing Constitutional Review laws in November. President and Makinda want to make sure CCM members are rewarded and keep the same pace on the next step to pass the new constitution . It is believed, there are a chance some members within CCM could defaulted the whole system preventing the new constitutional process to get stack a long the way. the only way is to please these unhappy members by giving posho to everyone, Unfortunately, it back fire, and it made CCM look more worse than ever, they cast another ugly image before the public - UNTRUSTED PARTY THAT CAN NOT BE TRUSTED.

    ReplyDelete
  10. siasa za maji taka ndo hizo,kupurukuka,spika alihamasishwa na wabunge wake wa ccm,akaona watampiga chini,yale si maamuzi ya kichwa kilichotulia kama cha sita.yule mama watampelekesha hadi atie akil.2015 hatautamani ubunge hata,labda vt maalum vya bure,na katiba hii hakuna viti maalum vya bure,ni ujinga,kama kuna fungu la pesa za bure kama za rada malizeni matatizo ya waalimu,boresheni shule za msingi na za kata,acheni uvivu wa kufikiri!!.

    ReplyDelete
  11. Hongereni mnaopinga nyongeza ya posho za Wabunge lakini zingatieni Jambo serikali ya CCM inajidhalilisha. Serikali ni CCM, katiba ni CCM, na Bunge kwa sasa ni la wapiga makofi wa CCM. Hoja za nguvu zimewashinda na mambo yao ndiyo hovyo kabisa. Wengi kwanza wanalala tu Bungeni hakuna wanachofanya zaidi ya kupiga makofi. Itafika siku tutawakataa. shauri lenu.

    ReplyDelete
  12. Mimi ninachofikiri Spika tulie nae hana haoni mbali kwani inashangaza kuona mama mtu mzima anakaa kwa waandishi wa habari na kutetea wabunge walipwe laki mbili kwa siku bila kufikiri maisha ya watanzania walio wengi wanaishi chini ya dola moja, kweli hili linaingia akilini, kweli inasikitisha mama kukosa huruma na mtizamo......Mungu ibariki Tanzania tupate viongozi waadilifu na waona kesho itakuwaje..............

    ReplyDelete
  13. kUNA MDAU KASEMA VIZURI - TUBADILISHE HAYA MAFISADI - CCM CHINI PWA!! HALAFU MTAONA JINSI MABADILIKO YATAKAVYOKUWA.

    HAMUONI TU HATA HAPO NCHI JIRANI - TANGU KANU IONDOKE MADARAKANI MMESHUHUDIA JINSI UCHUMI WA KENYA UNAVYOENDESHWA? WACHILIA MBALI POST ELECTION VIOELENCE - THAT COUNTRY IS BEING MANAGED -SIYO BLAH BLAH ZILIZOKUWA ZA KANU.

    HAPA KWETU ccm SIYO TU BLAHA BLAH, BALI INATUFANYA KABISA ...TUIPIGE CHINI MUONE,. ACHENI KUOGOPA MABADILIKO!!!!!!!!

    ReplyDelete
  14. rais na watendaji wake ni wala rushwa inatakiwa wakamatwe na kuwekwa jela haraka

    ReplyDelete