24 January 2012

Wafanyabiashara wadaiwa kutumia leseni za wenzao

Na Theonestina Juma,
Bukoba

WAFANYABIASHARA wasio na leseni ya biashara ya kahawa wanadaiwa kufanya biashara ya zao hilo mkoani hapa kwa kupitia mgongo wa leseni za wafanyabiashara wa kahawa wenye kibali hicho.


Hayo yamebainishwa katika taarifa ya Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya COOPedec,Bw. Jovin Banturaki, ilioteuliwa na Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko kufanya kazi ya mshauri mwelekezi juu ya uanzishaji wa mfumo wa stakabadhi za maghala kwa wakulima wa kahawa mkoani hapa.


Alisema wafanyabiahara hao kupitia mgongoni  mwa walio na leseni wamekuwa watafutaji wa kahawa vijijini, ambapo hupita nyumba hadi nyumba kununua kahawa bila kujali ni aina gani iwe hata ambayo  bado ipo katika mti  haijavunwa hulangua tu.

Alisema watu hao hupata fedha za kununulia kahawa ya agendo kutoka kwa wafanyabiashara wa magendo hata kwa wale wenye leseni huku baadhi yao nao wakipata kutoka kwenye vyama vya ushirika.


Bw. Banturaki alisema kufuatana na hali hiyo, wakulima wametumbukizwa katika dimbwi la umasikini kutokana na kulazimika kuuza kahawa kwa bei ya chini bila vipimo vya mizani.

Alisema kuwepo kwa njia haramu ambayo imeenea mkoa mzima, uharibifu mkubwa tayari umekisha rekodiwa na hivyo kusababisha athari kama hali mbaya ya kiuchumi na kifedha kwa wakulima wa zao hilo, huku ubora wa kahawa nayo ukififia.


Aidha magendo ya kahawa kwenda nje ya  mipaka ya nchi  huku ushuru wa kahawa hiyo ikiwa hailipwi katika halmashauri za wilaya na hivyo kuzikosesha mapato muhimu kutokana na ndiyo zao tegemeo la mkoa huu.



Hata hivyo, akizungumzia juu kutambua na kuchambua changamoto zilizopo katika mauzo ya zao hilo mkoani hapa ni pamoja na kuweka kikundi cha kuhakikisha takwimu sahihi zinapatikana na zinakusanywa manunuzi ya kahawa vijijini yanafanywa na wafanyabishara binafsi.


Pia alibainisha kuwa  ni pamoja na uelewa juu ya mambo gani yanayofanikisha thamani ya kahawa, kufanikisha uanzishwaji wa mfuno wa stakabadhi wa maghala na kusitisha biashara ya magendo ya kahawa kuvuka mipaka ya nchi na ulazimishaji wa kufuata kanuni zinazotawala mauzo ya kahawa pia imekuwa miongoni mwa athari.

No comments:

Post a Comment