27 December 2011

Papic avunja ukimya Yanga

*Adai uongozi unamtenga
Na Zahoro Mlanzi

KOCHA Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic ameamua kuweka wazi kinachoendelea ndani ya klabu hiyo, baada ya kusema kama hazijafanyika jitihada za
dhati timu hiyo itakwenda pabaya.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Papic alisema amekuwa akipata wakati mgumu kujibu maswali ya waandishi kuhusu mambo mbalimbali ya klabu hiyo, hivyo kutokana na hilo ameamua kueleza kinachomkera.

Alisema pamoja na taifa kukumbwa na janga la mafuriko, timu hiyo haijafanya mazoezi kwa wiki moja sasa kutokana na sababu mbalimbali ukiachilia mbali mafuriko.

“Kitu kikubwa kinachoisumbua Yanga ni ukata, timu haina hela kabisa ukiangalia hata hela nilizoomba kwa ajili ya 'gym' mpaka leo sijapewa, wachezaji wanadai mishahara lakini hakuna kinachoendelea.

“Wakati mambo hayo yakiendelea nilijaribu pia kuomba fedha ili niende na timu ufukweni, pia nazo kimya sasa nashangaa timu itajiandaa vipi na huku tuna mashindano mbalimbali,” alisema.

Alisema anafanya kazi katika mazingira magumu, alafu mwisho wa siku mashabiki na wanachama wanataka matoke mazuri, katika mazingira hayo hatutaifunga Zamaleki labda itokee miujiza.

Aliongeza kwamba kutokana na hali hiyo, hadhani kama mechi za kirafiki za kimataifa zitapatikana kitua ambacho jambo kinamkatisha tamaa, huku viongozi wakionekana kuwa mbali naye.

Alisema inafikia hatua klabu inakosa hata fedha za mafuta kwa ajili ya gari lake, ambapo analazimika kutoa fedha zake kwa ajili ya klabu.

Mbali na hilo, aliwaomba wadau, wanachama na mashabiki wa timu hiyo ambao huisaidia, wajitokeze kutoa msaada kwani klabu ipo katika hali mbaya kifedha.

No comments:

Post a Comment