27 December 2011

Ilala marufuku 'Disko Toto kimya

Na Mohamed Kazingumbe

HALMASHAURI ya Manispaa ya Ilala, Jijini Dar es Salaam, imepiga marufuku vibali vya 'Disco Toto' pamoja na maonesho ya 'Khanga Moja' katika kumbi zote.Akizungumza
Dar es Salaam juzi Ofisa Utamaduni wa Ilala, Shani Kitogo, alisema hatua hiyo inalenga kuepusha mmomonyoko wa maadili wa jamii.

Alisema hatua hiyo inawakumba wamiliki wa kumbi za starehe, baa, kutowaruhusu watoto chini ya miaka 18 kuingia kwa kisingizio cha kufuata kununua soda au juisi, vitendo ambavyo vinachangia ushawishi wa ukiukwaji wa maadili ya Mtanzania.

Ofisa huyo alisema agizo hilo ni la siku nyingi, lakini lilikuwa linapuuzwa na wamiliki wa utoaji wa huduma hiyo, sasa limevaliwa njuga.

"Hata baadhi ya vyombo vya habari vinatakiwa vilaumiwe kwa kukubali kutangaza matukio kama ya 'Kanga Moja' na kuremba sana hali ikieleweka maonesho yenyewe ni kinyume cha utamaduni wetu," alisema.

Alisema hatua hiyo pia, inapiga marufuku wazazi kuingia na watoto wao ndani ya kumbi za starehe ambako baadhi yao, wanaingia na watoto huku wenyewe wakinywa pombe na watoto kupewa soda.

No comments:

Post a Comment