27 September 2011

Lampard hatihati Chelsea

LONDON, Uingereza

HATIMA ya baadaye ya kiungo Frank Lampard, katika Chelsea imeanza kuwa kwenye hatihati baada ya kuachwa kwenye mechi na kutoka nje ya Uwanja wa
Stamford Bridge.

Nyota huyo mwenye umri wa miaka 33, aliwekwa benchi na hakutumiwa katika mechi ya Ligi Kuu England ambayo Chelsea, ilishinda mabao 4-1 dhidi ya Swansea.

Kitendo cha kutoka nje ya uwanja, wakati amewekwa kwenye benchi kimemkasirisha kocha wa timu hiyo, Andre Villas-Boas.

Kwa mujibu wa The Suna, Lampard aliondoka uwanjani na kwenda kwenye chumba cha kubadilishia jezi, kabla ya kuisha kwa mechi baada ya kocha kumpanga mchezaji kinda Josh McEachran, kuchukua nafasi ya Raul Meireles dakika ya 83.

Kiungo huyo kama angecheza katika mechi hiyo, angefikisha idadi ya mechi 350 katika Ligi Kuu tangu alipojiunga na Chelsea 2001 kwa ada ya pauni milioni 11, akiktokea West Ham.

Lampard sasa ameshaachwa kwenye benchi katika mechi tatu, kati ya nne za Chelsea, katika mechi dhidi ya Manchester United ambayo timu yake ilifungwa mabao 3-1, alitolewa baada ya kuisha kipindi cha kwanza.

Villas-Boas alisema Lampard, hakupaswa kukasirika na kama ilivyo kwa wachezaji wengine anapenda kuanza kucheza.

Alisema Lampard ni mchezaji mzuri, ana kipaji cha kipekee na kwamba atarejea kwenye kikosi chake haraka.

Kocha huyo alisema hakumchezesha Lampard na wengine kwa kuwa Jumatano, baadhi ya wachezaji walicheza kwa dakika 120 katika mechi ya michuano ya Kombe la Ligi.

Kama Lampard atapoteza namba katika kikosi cha Chelsea, ina maana hata kocha Fabio Capello anaweza kuacha kumwanzisha kwenye timu ya England.

Kocha huyo wa kitaliano, amekuwa akimwanzisha  Scott Parker na Jack Wilshere wanapokuwa fiti.

Kasi na mwelekeo wa Lampard katika kupasia umekuwa ukihojiwa wakati kocha Villas-Boas, amekuwa akitaka kuongeza kasi katika timu yake.

Kocha huyo Chelsea, amekuwa akisaka msaidizi wa Fernando Torres, ambapo amempa jukumu la kumsaidia kiungo mpya aliyemsaini msimu huu Juan Mata.

Torres ameanza kufunga magoli, lakini katika mechi iliyopita alioneshwa kadi nyekundu kutokana na kumchezea rafu, Mark Gower wa Swansea.

Lampard ni mchezaji wa nne, kati ya waliocheza mechi nyingi za kuanza katika Chelsea, akiungana na Ron Harris, Peter Bonetti na John Hollins.

No comments:

Post a Comment