15 August 2011

Mil. 30/- zatengwa kujenga viwanja vya michezo

Na Anneth Kagenda

ZAIDI ya sh. milioni 30 zimepangwa kutumika kwa ujenzi wa vitu mbalimbali vya maendeleo vikiwemo viwanja vya michezo tofauti tofauti kwa ajili ya kuhamasisha
vijana kushiriki mashindano yoyote yatakayokuwa yakitokea.

Akizungumza na gazeti hili Dar es Salaam juzi, Diwani wa Kata ya Bunju, Majisafi Sharif alisema  uwanja huo ambao tayari maandalizi yake ya kujengwa yameshaanza na sh. milioni 6 kati ya hizo zitakarabati barabara kwa kuweka kifusi.

Alisema barabara hizo ni ile ya Magereza na Bunju kwa kuweka kifusi ili kuziba mashimo makubwa yaliyopo na hivyo kupunguza usumbufu uliojitokeza kwa wananchi wake na uwanja mmojawapo wa michezo ukiwa ni ule wa Bunju A.

Alisema kata yake imekuwa na tatizo la kuwepo na viwanja vya michezo kwa vijana hivyo analenga kufanya maboresho ili vijana na watu wengine waweze kuvitumia.

"Tunavyojua michezo ni sehemu mojawapo ya mazoezi kwa vijana wetu na watu wazima hivyo vikishakamilika itakuwa ni sehemu ya maendeleo kwa wananchi wangu," alisema Sharif.

Alisema msaada wa fedha hizo ni kwa kushirikiana na Taasisi ya Jambo Real Estate Agent ambayo imejitolea kusaidiana naye kwa ajili ya maendeleo ya watanzania.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, James Ndika alisema taasisi yake imekuwa ikijishughulisha kwa kufanya shughuli za kuwaletea maendeleo wananchi pamoja na zile za kujenga na kuuza nyumba na kwamba hawajaanzia kwa diwani huyo bali hata maeneo mengine wamekuwa wakitoa misaada ya ujenzi wa viwanja mbalimbali.


No comments:

Post a Comment