06 July 2011

Hosea anga'ang'aniwa ajiuzulu

Na Grace Michael, Dodoma

MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Dkt. Edward Hoseah ametakiwa kujiuzulu kazi hiyo kama anaona
imemshinda.

Ametakiwa kufanya hivyo endapo anashindwa kutimiza majukumu yake kutokana na shinikizo la viongozi wa ngazi ya juu serikalini hatua inayokwamisha nia ya dhati ya kupambana na vita ya rushwa hasa kwa wala rushwa wakubwa.

Dkt. Hoseah alipewa changamoto hiyo jana na wabunge mbalimbali hasa wa kambi ya upinzani, wakati wakichangia hotuba ya Bajeti ya mwaka huu wa fedha katika Ofisi ya Rais Menejimenti na Utumishi wa Umma.

Mbali na TAKUKURU, wabunge hao pia wamekitaka Kitengo cha Usalama wa Taifa kuachana na utamaduni wa kudhibiti vyama vya upinzani na badala yake wajielekeze katika kazi zinazohusu maslahi ya nchi.

Akichangia masuala hayo, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa alisema kuwa haina maana kwa Mkurugenzi huyo wa TAKUKURU kuendelea na kazi huku akikumbana na vikwazo vya kazi kutoka kwa wakubwa wake.

Alisema kuwa ameshangazwa kuona serikali haina mkakati wowote wa kuongeza meno zaidi kwa TAKUKURU katika utendaji wake ilhali ikijua wazi kuwa taasisi hiyo ina vikwazo vingi katika kutekeleza majukumu yake hasa kuwashughulikia wala rushwa na watoa rushwa wakubwa.

“Nasema hivi kama Bw. Hoseah anaona kazi ina vizuizi vingi na hawezi kuifanya basi awarejeshee kazi yao kwani kuendelea nayo haina maana...na kama Hoseah alikiri mwenyewe kuwa hawezi kufanya mambo mengine kwa kuogopa kushughulikiwa basi aikatae kazi yao,” alisema Mchungaji Msigwa na kuongeza kuwa.

“Alipopokea kazi hii alitakiwa kuifanya na asipoifanya basi atueleze ni nani anaifanya, hatuwezi kuwa na kiini macho kuwa kuna kitengo cha rushwa huku hakifanyi kazi, imefikia mahali hata kwenye kugombea watu wanakimbizana kwa kuwa wameahidiwa uwaziri na hapa wanakimbilia kwa kuwa uwaziri ni dili na sio kwa maslahi ya wananchi hivyo hatuwezi kuwa na kitengo kisichokuwa na meno hata kidogo,”alisema Mchungaji Msigwa.

Kutokana na hali hiyo, aliitaka serikali kutoa majibu ya namna gani kitengo hicho kitaboreshwa ili kupambana na rushwa ambayo imekuwa ni adui mkubwa wa haki za wanyonge.

Akizungumzia suala la Usalama wa Taifa, alisema kuwa yeye binafsi anaamini kitengo hicho kimeacha kufanya kazi zake na kujikita katika kazi ambazo hazina maslahi ya Taifa kama kinavyotakiwa kufanya.

Alisema kuwa kitengo hicho kwa sasa kimejikitaka katika kazi ya kuvidhibiti vyama vya upinzani badala ya kutetea maslahi ya wananchi hatua inayosababisha kila mambo kwenda kama yanavyotaka.

“Imefika mahali wanyama wanaibiwa huku usalama wa Taifa wakiwa kimya, misitu inaondoka wapo tu kimya, tunataka yafanyike mabadiliko katika chombo hiki ili kiwe kwa ajili ya maslahi zaidi ya taifa...ili waokoe nchi yetu, waende nje wakaibe namna wenzetu wanafanya kazi na kukuza uchumi, wafanye ujasusi wa kiuchumi na siyo hayo mambo wanayoyafanya kwa sasa ambayo hayana tija kwa nchi,” alisema Mchungaji Msigwa.

Alisema kuwa kutokana na kuacha kazi, imefika mahali wanyama wanaibwa na kusafirishwa hadi nchi za nje huku waziri husika akiwa kimya bila hatua zozote hivyo akaomba viongozi kuwa na utamaduni wa uwajibikaji.

Naye Mbunge wa Singida Mashariki, Bw. Tundu Lissu, akichangia suala la utendaji wa TAKUKURU, alisema kuwa kama chombo hicho hakina uwezo wa kuchukua hatua kwa wala rushwa wakubwa basi taifa liko katika hatua mbaya zaidi.

“Kama maneno aliyosema Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU kwa Maofisa wa Kibalozi wa Marekani ni kweli kwamba tatizo la rushwa kubwa linashindikana kupatiwa dawa kwa sababu uongozi wa juu wa nchi hii unazuia, basi taifa hili tumefika mahali pabaya.

“Haya ni maneno ambayo yako katika diplomatic cables za Ubalozi wa Marekani kwenda Washington DC, kwenda State Department ya Tanzania, according to Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU kwamba Serikali ya Tanzania tunashindwa kuchukua hatua kwa sababu Uongozi wa Juu wa Kitaifa unatuzuia. Hili tatizo ni kubwa. Si tatizo la kisheria tena,  kwa sababu kwa sheria ya TAKUKURU ya mwaka 2007 yale Mamlaka ya Rais, kumuelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa TAKUKURU kitu gani afanye na kipi asifanye hayapo tena,” alisema Bw. Lissu.

Alisema kuwa suala hilo ni zito na kama Taifa kuna haja ya msingi ya kupambana nalo ili rushwa kubwa ziweze kushughulikiwa.

“Bado tuna tatizo la kwamba asipofanya wanavyotaka hata kama sheria haimsemi afuate maneno yao, asipofanya anapoteza kazi au ataachishwa kazi, Sasa hili ni tatizo kubwa kama taifa tuna wajibu mkubwa wa kupambana nalo, kwa namna yoyote ile inayowezekana kama haiwezekani kwa namna hizi za kawaida wananchi watachukua namna zingine ambazo siyo za kawaida,” alisema Bw. Lissu.

Alisema kuwa endapo wananchi watachoshwa na hali hiyo kwa muda mrefu uvumilivu utawaishia na watachukua hatua ambazo hazijazoeleka zikiwemo za kuingia barabarani.

10 comments:

  1. Safi wapiganaji wa Chadema! Mimi nawapenda wapinzani particularly Chadema. SIMPLY, Wanaongea hoja mzito!

    ReplyDelete
  2. Mimi nilimshangaa MB wa viti maalumu Munde Tambwe kutetea TAKUKURU, lakini kilichonishangaza zaidi ni pale alipoponda TEKNOHAMA kwamba watanzania tuipuuze kwamba itatuchonganisha. alikuwa aki-refer wikileaks.

    These are stupid words I had never heard in this century. Wakati dunia inakimbia kwasababu ya hii technologia leo Mbunge anasema tuipuuze?! Huyu Munde anataka tuishe tena kama enzi za STONE AGE? Ana matatizo ya akili aende Milembe.

    Lakini matatizo ya wabunge wa aina ya Munde ni hivi VITI MAALUM?! I swear to my dead body mimi nitapigana kufa KATIBA MPYA tusiwe na wabunge wa VITI MAALUM.

    ReplyDelete
  3. nakusahihisha kidogo,ujinga wa upeo si viti maalumu ni ujinga wa ccm,wewe angalia hata mawaziri upuuzi wanaoongea,lkn suzan lyimo ni kiti maalumu na akitoa hoja huwa nzito zaidi ya hata za waziri mkuu,la msingi ni kuondoa viti maalumu kwa ujumla labda tuache kwa watu maalumu kama walemavu tu.

    ReplyDelete
  4. sasa anon hapo juu ukiweka vya walemavu tu si ndo CCM watakomba vyote maana naapa mbele za Mungu safu yote ni walemavu wa akili,haiingii akilini wanavyootetea upuuzi hata mwanangu wa miaka miwili anaweza kukupa majibu

    ReplyDelete
  5. Jamani tuache kumsema Dr. Hosea kuhusu rushwa. Rushwa ni kama kansa kwetu, kuithibiti inabidi taifa zima libadirike. Ni nani ajapewa, ona, au ajasikia fulani kapewa rushwa kwa wadhifa wake? Yaani sasa inabidi turidi wakati wa Nyerere, kufundisha Ethics 101, kwa hiyo mtu anajisikia vibaya yeye mwenyewe.

    ReplyDelete
  6. Kinachowasumbua watanzania wengi katika suala la rushwa ni wivu,kwamba kwanini na wao hawajawekwa kwenye nafasi zitakazo wawezesha kula rushwa,hata hao wanaojifanya kupigia kelele rushwa wakiwekwa kwenye nafasi izo watakula tu.Angalia PCCB,huu ni upande wa shilingi ambao watu hawataki kuuangalia na kujiridhisha kuwa PCCB wako kwa ajili ya kupiga vita rushwa,sio kweli,kwa utafiti niliofanya taasisi inayoongoza Tanzania kwa kula rushwa ni PCCB,hao kwa sasa ndio wanaoongoza kwa kuwa na majumba ya kutisha,magari ya nguvu,fedha kibao,nk hii ndio maana wanakamata watendaji,makarani wa mahakama za mwanzo,polisi wadogo,mahakimu wa mahakama za mwanzo ,waalimu na wale wote ambao hawana mshiko wa nguvu,thubutu uwezi sikia meneja wa TRA kakamatwa,engeneer wa TANROAD, Waweka hazina wa mikoa na halmashauri,ma DC kwani nao wamo kwa rushwa za wawekezaji,Ma RPC,RTO,etc,hivi PCCB mnapokamata hao maskini kwa rushwa ya elfu 10 hamuoni aibu,roho zenu haziwasuti,kwanini msihoji hao watendaji wenye utajili wa kutisha ni wapi wamepata izo pesa au hiyo mitaji wakati hawajawahi kukopa benki na mishahari yao tunaijua?

    ReplyDelete
  7. mi nadhani watanzania tunaigiza ktk mambo mengi tena hasa yale ya msingi,hivi nani asiyejua kuwa rushwa inayozunguzwa tz ni ile tu ambayo haiwahusu "wenzetu?"kuna kesi ngapi mahakamani ambazo zinawahusu "wenzetu"mpaka sasa?huyu huyu bwana hosea ana ujasiri gani leo wa kusimama na kukemea rushwa?ni ripoti ngapi zimetoka na kumhusisha yeye binafsi na rushwa!ripoti ya mwakyembe ni moja wapo.kilichobaki sisi watanzania tukubali tu rushwa,kutowajibika,ubinafsi,uzembe na uporaji wa mali za umma ni sehemu tu utamaduni wetu kama zilivyo tamaduni zetu zingine,unyago,jando,ngoma n.k
    kwa kweli haya mambo yanatia HASIRA sana kwa watu tuliowapa dhamana ya kusimamia mambo yetu huku wakitumia kozi zetu kubwa kuzigeuza mali zao binafsi.
    lakini wakae wakijua watanzania tunajua kila kinachoendelea wala wasidhani huo "welevu"wao ndiyo "ujinga" wetu au wasidhani suti zao za bei mbaya zinawapa wao haki ya kujiona bora sana kuliko sisi na mitumba yetu,nchi hii ni yetu sote.

    ReplyDelete
  8. TAKUKURU haiko huru ,kama kiongozi wake anchaguliwa na Rais ni sawa na mwenye mbwa akimuamuru mbwa shika! atashika ,acha ata acha.Ndio sawa na Hosea.HAKUNA NIA YA DHATI KUTOKOMEZA RUSHWA KWA SERIKALI

    ReplyDelete
  9. Mimi napendekeza kuwa hiki chombo (TAKUKURU) KIFUTWE. kwanza licha ya kuwa kinalinda na kuwasafisha wabadhilifu wakubwa, kimeonyesha pia hakina ufanisi kabisa. Takwimu zilizopo zinaonyesha ni asilimia moja tu (1%) ya kesi zilizosimamiwa na TAKUKURU ndiyo zilizo patikana na makosa.Asilimia 99 (99%)TAKUKURU ilishindwa kwenye kesi zake. Sasa kama BUNGE linataarifa hii na madudu mengine, inatosha kabisa kuiambia serikali ifute kitengo hiki maana hakina manufaa kwa Taifa na kinatumia kodi zetu bure badala tungepeleka maeneo mengine muhimu yenye mapungufu makubwa. Hivyo haitoshi Dr. Hossea pekeyake kujiuzulu, bali hata TAKUKURU ifutwe.

    ReplyDelete
  10. Kila mmoja wetu anajukumu kuondoa rushwa. hata kama ni hii rushwa inayoitwa ndogondogo. wangapi wanatoa rushwa kwa traffic barabarani? tuache wote kutoa rushwa. hata kama haki inachelewa, tusubiri, tusitoe rushwa.

    ReplyDelete