09 May 2011

CHADEMA wamtaka Dk. Mwakyembe ajiuzulu

*Ni kwa serikali kugomea mapendekezo yake ya Richmond
*Washangaa Rais Kikwete kuwapa madaraka aliowatuhumu
*Wasema akijiuzulu atalinda uadilifu na heshima yake

Na Tumaini Makene

MZIMU wa sakata la kampuni tata ya Richomond, umezidi kuwaandama wanasiasa nchini, sasa
ikiwa ni zamu ya Naibu Waziri wa Ujenzi, Dkt. Harrison Mwakyembe ambaye ametakwa kujiuzulu kutoka serikalini ili kutunza uadilifu wake baada ya serikali kupuuzia maagizo ya Kamati Teule ya Bunge iliyochunguza sakata la kashfa hiyo.

Ameambiwa kuwa iwapo ataendelea kung'ang'ania kubaki katika serikali ya namna hiyo, atakuwa anafanya hivyo kwa sababu ama ya 'uroho na ulafi' wa madaraka au kutokuwa na uwezo wa kusimamia misimamo ya uongozi adilifu, tofauti na Watanzania wengi wanavyomwelewa.

Hayo yalisemwa jana na mmoja wa makada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Fred Mpendazoe, ambaye katika bunge lililopita kabla hajajiuzulu ubunge wake wa Kishapu alikuwa ni mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini.

Akizungumza katika mikutano ya Operesheni Sangara ya chama hicho katika Nyanda za Juu Kusin, mkoani Mbeya, amesema kuwa Dkt. Mwakyembe ndiye alikuwa mwenyekiti wa kamati hiyo teule ya bunge, ambayo katika moja ya mapendekezo kwenye ripoti yake, ilitaja watendaji wa serikali waliohusika katika kashfa hiyo, mmoja wao akiwa ni Bw. Bashir Mrindoko, ambaye wakati wa sakata la Richmond, alikuwa ni Kamishna wa Nishati, katika Wizara ya Nishati na Madini.

Bw. Mrindoko ambaye hivi karibuni aliteuliwa na Rais Kikwete kuwa Naibu Katibu Mkuu katika Wizara ya Maji, alikuwa kwenye orodha ya kamati ya Dkt. Mwakyembe ikipendekezwa achukuliwe hatua za kinidhamu kwa kushindwa kumshauri Katibu Mkuu mpya wa Wizara kuhusu udhaifu wa Richmond Development Company LLC.

Bw. Mrindoko ndiye aliyeiandikia barua kampuni hiyo kusitisha mkataba wake na serikali mwezi mmoja tu kabla ya mchakato wa zabuni ya umeme wa dharura haujaanza.

"Mwakyembe anapaswa kujiuzulu ili kulinda hadhi yake ya uadilifu kama wananchi wengi wanavyomjua, hakuna haja ya yeye kuendelea kuwa katika serikali ambayo haiheshimu mapendekezo ya kamati yake ambayo bunge liliyaazimia...lakini kama ataendelea kung'ang'ania kubaki ndani ya serikali ataonekana ni mroho wa madaraka au hana msimamo thabiti katika kusimamia misimamo ya uongozi adilifu," alisema Bw. Mpendazoe.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Bw. Kabwe Zitto, aliwaambia wananchi katika mikutano yake kuwa chama hicho kimepanda chati kwa asilimia 400, kati ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 na 2010, kwani kabla ya uchaguzi wa mwaka jana kilikuwa na madiwani 101 sasa wameongezeka kufikia 466, huku wabunge wakiongezeka kutoka 11 mpaka 48.

Huku akiwataka wananchi kuendelea kujipanga kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao, kuhakikisha chama hicho kinashinda na kuchukua dola, Bw. Zitto alisema kuwa mgombea urais wa CHADEMA uchaguzi mkuu mwaka jana, Dkt. Willibrod Slaa alishinda lakini matokeo yake 'yakachakachuliwa'.

Aliwashukuru wananchi kwa kuendelea kukiunga na kukipandisha chati chama hicho ndani ya muda mfupi hata kumpatia kura nying 'za ushindi' Dkt. Slaa, akiwataka waendeleze moyo huo wakijipanga zaidi kwa uchaguzi mkuu ujao.

Wakati huo huo imeelezwa kuwa ufisadi mkubwa ikiwemo rushwa na ukosefu wa uwajibikaji wa serikali kwa watu wake umesababisha kuyumba kwa uchumi wa nchi na kumilikiwa na watu wachache, huku Watanzania wengi wakiachwa kando wakigubikwa na umaskini unaochangiwa na makali ya maisha yanayoonekana kuongezeka kila siku.

Hali hiyo imesababisha 'mahubiri' ya amani miongoni mwa Watanzania kutokuwa na uhalisia wowote, ikidaiwa kuwa mtu asiyekuwa na uhakika wa kupata haki ya mlo, elimu na matibabu bora hawezi kuwa na amani ya kweli, katikati ya utajiri wa raslimali zilizoko nchini.

Hayo yamesemwa na Mbunge wa Viti Maalum (CHADEMA), Bi. Chiku Abwao katika mikutano ya maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Mbalizi, mmkoani Mbeya katika mikutano yake mbalimbali ya Operesheni Sangara kwa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.

Alisema kuwa chama hicho hakitakubali Watanzania waendelee kufanyiwa dhuluma na viongozi wao wenyewe, ambao wamesahau kuwa uongozi ni dhamana ya kuwajibika kwa watu wala si kujinufaisha au kujineemesha binafsi.

"Umaskini tulionao si wa kurogwa wala hatukuumbiwa na Mwenyezi Mungu, ni matokeo ya kukosekana akwa uongozi unaowajibika kwa maslahi ya wananchi wake wanaolipa kodi kila siku lakini kodi hiyo haionekani ikirudi kwa kwao kwa maana ya huduma za kijamii.

"CHADEMA hatuwezi kuvumilia hali hii, ndiyo maana safari hii tumejipanga kupambana vilivyo bungeni kuhakikisha serikali inawajibika kwa wananchi wake hasa katika suala la kukuza uchumi na kupunguza umaskini wa Watanzania.

"Hali ya wananchi inazidi kuwa mbaya, umaskini na ukali wa maisha unazidi kuongezeka kila kukicha, lakini hakuna mikakati imara na mahsusi kuhakikisha mwananchi anapata nafuu ya maisha. Tunataka serikali ishushe bei ya umeme na pia sehemu ambazo umeme haujafika ufikishwe, ili wananchi wapate nafuu ya maisha...suala la nishati ni muhimu sana katika maendeleo ya uchumi wa nchi na mwananchi mmoja mmoja.

"Hivi majuzi tumeandamana huko Mwanza mkamsikia Rais Kikwete akiagiza sukari ishuke bei mpaka sh. 1,700 lakini mpaka leo hakuna uhalisia katika agizo lake hilo, sukari pamoja na bidhaa nyingine muhimu kwa wananchi zinazidi kupanda...anatoa agizo akisahau kuwa mahali sahihi pa agizo lake hilo ni bungeni ambako serikali inaweza kushusha kodi za baadhi ya bidhaa na huduma ili kumpatia ahueni ya maisha Mtanzania maskini," alisema Bi. Abwao.

Kwa upande Mkurugenzi wa Usalama na Ulinzi wa CHADEMA, Bw. Wilfred Lwakatare alisema kuwa vitendo vya ufisadi vinavyoachiwa kutamalaki kuanzia ngazi ya chini katika serikali za mitaa mpaka serikali kuu ni moja ya chimbuko la kuyumba kwa uchumi wa nchi unaomilikiwa na watu wachache, hivyo kusababisha wananchi wengi kutengwa, wakiendelea kugubikwa na umaskini unaodhihirika katika ukosefu wa kipato na huduma za msingi za jamii.

Alisema kuwa kwa jinsi hali ya uchumi inavyozidi kuwa ngumu imefikia mahali hata vijana hawataki kuwa na familia kwa maana ya kuoa na kuolewa kwa hofu ya kushindwa kumudu maisha ya kuhudumia familia.

5 comments:

  1. Watanzania tuwaunge mkono ,HIYO NDIO KAZI YA VYAMA VINGI sasa ndugu zangu wanaandika maoni kwa matusi.
    KUANDIKA KUTOA MAONI KWA MATUSI NI KUONYESHA KUWA SISI WATANZANIA 80% HATUJUI MABAYA NA MAZURI,MUHIMU changia maoni yako kwa kusema maneno mazuri au mabaya yanayofanywa na chama au vyama.
    TANZANIA NA DUNIA YA LEO INAHITAJI MAGEUZI NA KUZUNGUMZA UKWELI NDIO SILAHA YA WANYONGE,ila kwetu Tanzania kuwadangaya wananchi ndio furaha ya watu kwa kutegemea utajili wa haraka kumbe ni ndoto za mchana

    ReplyDelete
  2. 1) Hakuna sababu ya Dr. Mwakyembe kujiuzulu. Yeye ni mwadilifu na ndio maana Rais kamteuwa na kumpa Wizara nyeti ashirikiane na Waziri anayewajibika John Magufuli. 2)Tujue kuwa Makyembe ni mwana CCM so ni haki yake kuitumikia Serikali ya CCM kama yatamshinda basi aamue mwenyewe kuachia ngazi. Tumpe Mwakyembe muda aonyeshe uwezo wake wa kuhudumia watanzania kwa uadilifu alioonyesha wakati akiwa mwenyekiti wa kamati iliyofumua siri za Richmond.
    Chadema endeleeni kupambana wananchi tutachuja pumba na Ngano. 0713686821

    ReplyDelete
  3. CDM kumwambia mwakyembe ajiuzulu si kwamba utendaji wake ni mbaya hapana ni ili kulinda sifa kubwa iliyopewa na wanachi kwa ajili ya utendaji wake wa kazi ulivyo mzuri usije ukachafuliwa na baadhi ya watu mwishoe wakamuingiza mkenge naye akawa fisadi hilo ndo haswa CDM wanamaanisha

    ReplyDelete
  4. Binafsi sioni Sababu ya Mwakyembe kujiuzulu, Kikwete ni bosi wake, Mwakyembe alifanya kazi yake vizuri, Watanzania wenyewe tukakubali hata Mafisadi walikubali ndo maana Lowasa na wenzake waliachia ngazi. Uzembe wa Kikwete kutofanyia kazi mapendekezo mazuri ya watu haujaanzia hapo, Kama ni kujiuzulu kwa mwakyembe basi watu wengi watatakiwa kujiuzulu kitu ambacho sidhani kitakuwa na maana.

    Kuna njia nyingi za mapigano, Wapo wanaopigana wakiwa ndani wote tunawafahamu na wapo wanopigana wakiwa nje yote mapigano tu. Acha akinamwakyembe wapigane wakiwa ndani, ili CCM idhoofu haraka.

    Hivi ninyi mnafikiri waadilifu wote wakijiuzuru Nchi tuwaachia mafisadi watupu kitatokea nini? Pamoja na kuwa na kundi kubwa la mafisadi ndani ya serikali bado naamini hao waadilifu wachache ndo wanafanya hata tunamka asubuhi na kusoma magazeti bila ya hivyo Tanzania ingekuwa imeuzwa. Mimi ni mpenzi wa Chadema ila siungi mkono hoja ambazo naona hazijengi ndani ya chadema. Tunatakiwa kupmbana na CCM na utawala wake kwa kuangalia ni wapi patatupa nguvu na kuimarisha chama chetu cha chadema, Kuna hoja ambazo zimeanza kutolewa siku za karibuni na baadhi ya viongozi wa chama chetu cha Chadema ambazo zinatupa hofu sana wanachama wake hasa zile hoja ambazo zinonesha kuwa kuna hela za akina Rostam, Lowasa na Chenge zimeanza kupenyezwa Chadema. Matokeo yake ndo Hoja kama hizi za kuwachafua watu maarufu wanokubalika na Jamii nzima bila kujali itikadi za Chama. Ndugu zangu tuwe Macho.

    Leo hii nikiona mtu anampaka matope Mkwembe, magufuli, Sitta, Kilango na wengineo lazima naanza hofu na uwezo wake wa siasa. Unapojaribu Kubonda Jiwe kwa nyundo jaribu kuangalia ugumu wake vinginevyo unaweza kupoteza nguvu yako na umaarufu wako.

    ReplyDelete
  5. nyie majira acheni kuandika tabia ya kuliharibu gazeti lenu kwa kuandika udaku wa Osama bin Laden. mnapofanaya hivyo kama leo kwenye gazeti; mnaharibu heshima yenu.

    ReplyDelete