20 April 2011

TFF yazipiga mkwara klabu Ligi Kuu

Na Zahoro Mlanzi

SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limezipiga mkwara klabu za Ligi Kuu Bara kusajili wachezaji walio huru kwa mikataba na si vinginevyo.Hadhari
hiyo inatokana na tukio lililotokea msimu uliopita ambapo wachezaji Steven Marashi, Wisdom Ndlovu, John Njoroge na Ally Msigwa wa Yanga waliachwa na mpaka leo hawajalipwa fidia zao.

Suala hilo liliendelea mpaka kufika katika Kamati ya Sheria na Hadhi kwa Wachezaji ambapo kama hiyo iliiamuru Yanga, iwalipe na mwezi uliopita wachezaji hao walitishia kusimamisha usajili wa klabu hiyo mpaka walipwe fedha zao.

Akizungumza Dar es Salaam jana baada ya kuulizwa kuhusu pilika pilika za usajili zinazoendelea kwa timu mbalimbali nchini, Ofisa Habari wa shirikisho hilo, Boniface Wambura alisema usajili rasmi unaanza Juni 20, mwaka huu mpaka Julai 20.

"Kwa mujibu wa kanuni, kipindi cha usajili ni Juni 20 mpaka Julai 20, hivyo katika kipindi hicho klabu inatakiwa isajili mchezaji ambaye yupo huru au klabu yake imevunja mkataba naye.

"Pia ndicho kipindi ambacho klabu zinatakiwa kuweka wazi wachezaji inaowaacha, ili wasajiliwe na timu zingine na zihakikishe zinaingia nao mikataba," alisema.

Wakati huo huo, Wambura aliongeza kuwa timu ya taifa 'Taifa Stars', inatarajia kuondoka kesho kwenda Msumbiji kuumana na timu ya taifa ya nchi hiyo ikiwa na msafara wa watu 30.

Alisema wanatarajia kuumana na Msumbiji Jumamosi katika mchezo wa ufunguzi wa Uwanja wa kisasa wa michezo kama ulivyo wa Taifa, Dar es Salaam na kurudi Jumapili.

1 comment:

  1. Tatizo lipo kwa TFF kwasababu ilikuwaje waidhinishe usajili mpya bila ya kuhakikisha wachezaji husika wameshalipwa fedha zao?Hili ni jambo rahisi sana kukomeshwa ili lisijirudie tena.Hiyo hapo juu ni njia ya kwanza na ya pili ni kukata mapato ya timu husika katika michezo zake za ligi na kuwalipa wachezaji.Bila ya hivyo hili tatizo litaendelea kila siku.Sasa hiviyanga wanasema wana bilioni sita kwa usajili lakini kulipa haki za wachezaji inakuwa ni vigumu,Je hii maana yake ni nini?.TFF mnatakiwa mjirekebishe pia na kujuwa nini cha kufanya.Sio kuishia kuzungumza tu bila vitendo.

    ReplyDelete