21 April 2011

CUF yakana ufisadi wa mabilioni

Na Rabia Bakari

CHAMA cha Wananchi (CUF) kimedai kushtushwa na taarifa zilizotolewa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu ufisadi wa vyama vya siasa na
chama hicho kudaiwa kushindwa kuwasilisha hesabu za matumizi ya shilingi bilioni tatu.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari jijini jana, Naibu Mkurugenzi, Habari Uenezi Mahusiano na Umma, Bi. Amina Mwidau alisema kuwa taarifa hiyo ni ya uongo, na inalenga kukichafua chama hicho.

"Ukweli ni kwamba ruzuku ya chama ya kila mwezi haizidi milioni 133, hivyo kwa vyovyote vile kwa mwaka mmoja wa fedha haziwezi kuzidi bilioni 1.6/-, na maelezo kuwa chama chetu kulipwa bilioni tatu ni uongo mkubwa.

"CUF kimekuwa kinafunga hesabu zake kila mwaka kwa kutumia mwaka wa fedha unaoanzia kipindi cha Januari hadi Desemba, hivyo kudaiwa hesabu kipindi kinachoisha Juni 2010 ni kupotosha sera ya chama chetu," aliongeza.

Aliongeza kuwa hesabu za mwisho zilizokaguliwa ni za Januari 2009 hadi Desemba 31, 2009 ambazo ziliwasililishwa kwa msajili wa vyama Agosti 23, 2010.

Alidai kuwa hesabu zilizobaki zipo tayari na zitawasilishwa mara baada ya vikao vya bodi ya wadhamini.

"Ni dhahiri kuwa taarifa iliyotolewa na CAG bila kufanya utafiti na kuwasiliana na sisi, ili kupata taarifa sahihi kama inavyostahili, tunamtaka aje na ushahidi na kuutangazia umma iwapo ana uhakika kuwa CUF haijakaguliwa hesabu zake na kuziwakilisha kwa msajili wa vyama vya siasa," alisema.

Aidha, Bi. Mwidau alisema kuwa CUF kinatumia fedha za ruzuku kwa utaratibu sahihi, na ndio maana tangu kuanzishwa kwa chama hicho hakujawahi kutokea kashfa ya upotevu wa pesa au utumiaji wa pesa za chama kinyume na sheria na kanuni zilizowekwa kikatiba.

"Tunawaomba Watanzania wote waendelee kuiamini CUF, kama chama pekee kitakacholeta uchumi imara na kitakachodhibiti matumizi mabaya ya fedha za kama ambavyo ilani za uchaguzi za CUF kuanzia mwaka 1995 zimekuwa zikisisitiza.

5 comments:

  1. Aidha CUF au Mkaguzi wa Hesabu (CAG) wanatudanganya. Ili kuepusha mgongano wa ukweli, kwa nini hatuzitumii Mahakama kulinda heshima ya chombo kinacho husika?

    Jamii ina imani kubwa na CAG, kwa hio ripoti yake itabakia ndio ukweli.

    Ili CUF ijisafishe na tuhuma hizi, ingempeleka CAG mahakamani na ikithibitika wadai fidia kwa kukashifiwa chama chao.

    Hili litakuwa fundisho na itaamsha uwajibikaji.

    ReplyDelete
  2. CUF mmekula fedha zetu. Wajibikeni

    ReplyDelete
  3. Twashukuru mambo yamekwenda salama kwa upinzani pamoja na chama tawala kukubali kukaa meza moja na kula sahani moja pia.Lakini kuna wakimbizi walisababishwa na migogoro ya kisiasa ktk miaka ya nyuma, mbona hawazungumziwi au......? ikiwa nchi imekwenda salama kwa nini wahusika hawavuti picha na matukio yalio pita nyuma kwa kujaribu kutia viraka kwa guo lililonyambuka awali? tunaomba serikali na CUF hususan huko visiwani iwatafute vijana wetu waliojipenyeza ktk siasa na kuingia mtegoni bila kujua yalio usoni kwa udi na uvumba ili asilimia 20 ya furaha yetu ikamilike.Wazee wapenda amani

    ReplyDelete
  4. Kiukweli wakimbizi wamepita mikondo mizito, na wameona mengi,hususan wale walio kaa kule mji mkuu wa Somalia,Mogadishu.Samahani waze wapenda amani kabla hamuja taka maoni yenu yamwilike mungevuta nanyi picha ya mapigano ya kila sekunde huko Usomalini na wenenu kukaa kwao kimya huko kwa miaka takriban 10 ! je yayumkinika kuwapembejea kurudi hapa bure bure, hiyo ni busara.? Kwa ushauri wangu ningeomba CUF iwasamehe kwa kuwaengua ktk chama chao na serikali kuwafutia uraia wao kabisaa wasije wakawa wameiva kwa moto unaofukuta kwa kila sekunde huko Usomalini na kokote kwengineko.
    Muungwana kobe

    ReplyDelete
  5. Nyinyi Ma anonymous 2 wa mwisho msituzingue.

    Mada inazungumzia ripoti ya mkaguzi mkuu wa serikali na ufisadi wa chama cha CUF.

    Hizo hoja zenu hazina uhusiano na mada hii. ikiwa nyinyi ni maofisa au wakereketwa wa CUF musijaribu kuficha shutuma zilizotolewa kwa kubadilisha mada na kuleta hoja zisizohusu. Kuweni wa wazi.

    ReplyDelete