25 April 2011

Bila haki hakuna amani, viongozi wa dini wasema

Na Benjamin Masese

VIONGOZI wa madhehebu mbalimbali wameonya kuwa amani ya nchi haiwezo kuwapo ikiwa serikali, wanasiasa na matajiri wataendelea kuikanyaga haki ya Watanzania walio
wengi kwa manufaa ya wachache.

Vile vile walisema kuwa ongezeko la maadui wakubwa wa nchi kutoka watatu hadi kufikia wanne umekuwa mzigo mkubwa kwa serikali kuwaondoa haraka kutokana na viongozi walio wengi kutokuwa wadilifu katika sehemu zao za utendaji kazi wao.

Walitaja maadui hayo ni pamoja na ujinga, umasikini, maradhi na ufisadi.

Hayo yalisemwa jana na Mosinyori Julian Kangalawe wa Kanisa Katoliki na Mchungaji wa Kanisa la Menonite, John Magafu wakati wakizungumza katika kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na Shirika la Utangazi la Taifa (TBC1) juu ya sherehe ya pasaka na mtazamo wa amani ya nchi.

Mosinyori Kangalawe alisema kuwa nchi yoyote inayopata maendeleo lazima iwe imefaulu mtihani wa amani na kuongeza kwamba nchi za Afrika zinaonekana kufeli, huku watu wake wakiendelea kuugua na kupata maradhi mbalimbali kwa sababu ya kushindwa kuitumia zawadi ya amani kutoka kwa Mungu.

"Sisi viongozi wa dini tunahubiri kila siku juu ya amani na upendo na tulichogundua watu wanashindwa kujua kwa undani maana ya maandiko yaliyoandikwa kwenye biblia, unajua mtu akisha kuwa muovu hata kama akiombewa hatabadilika, ndio maana hivi sasa tunashuhudia baadhi ya viongozi wakiitwa mafisadi, na hao kila siku wanaingia makanisani lakini hawabadiliki.

"Kanisa linasaidia watu wamuelewe Mungu kwa kufanya matendo mema lakini cha ajabu hata Dar es Salaam hii penye kila huduma, watu wanafanya mauaji hadharani, ufisadi, wizi na wanapokea rushwa bila woga, binafsi naweza kusema Mungu ni upendo pia upendo ni hulka ya mtu, na upendo ni siri inatolewa na Mungu," alisema Monsinyori Kangalawe.

Mosinyoli aliwataka wananchi kuendelea na upendo na mshikamano wao uliokuwepo katika kipindi chote kwaresima na sio kurudi katika matendo maovu huku akisistiza Watanzania kubadilika.

Alitoa wito kwa kila mwananchi kufikiria kukemea vitendo vinavyofanywa na wanasiasa nchini hasa katika sehemu zao za kazi na kuwataka kubadilika kwa manufaa ya maendeleo yao.

Naye Mchungaji Magafu alisema kuwa pasaka ya mwaka huu imekuwa ya aina yake kwa sababu Tanzania imesheherekewa pamoja na sherehe za kuadhimisha miaka 47 ya muungano, hivyo ni kipindi cha kutafakari umhimu wake.

Bw. Magafu alisema kuwa asilimia kubwa ya jamii imebadalika kutoka katika misingi ya haki na kusababisha watu kutoaminiana, huku kazi nyingi zikifanywa kwa hofu, hisia na mitazamo tofauti hivyo kuleta makundi mawili ya masikini na tajiri.

Alisema kuwa hivi sasa kundi la wanyonge limekosa amani kutokana na kiminywa kwa haki, na kutoa mfano kwamba mtu anayejikita kuwasaidia masikini mara nyingi hutazamwa na mamlaka, wanasiasa na serikali katika hali isiyo ya kawaida huku kila mtu akiwa na matazamo tofauti.

1 comment:

  1. amani ni zao la haki, bahati mbaya watanzania ni mbumbumbu, wanaimbiwa amani huku haki zao zikiminywa.

    WATANZANIA AMKENI KUDAI HAKI

    ReplyDelete