15 February 2011

Nauli mabasi ya mikoani juu

Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafirisha wa Majini na Nchi Kavu (SUMMATRA) imeridhia kupanda kwa nauli za mabasi yaendayo mikoani
vitakavyoanza kutumika wiki ijayo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana kwenye vyombo vya habari, viwango hivyo ni baada ya kupitia maombi ya Chama cha Wamiliki wa Mabasi nchini (TABOA) ili kukabiliana na gharama za uendeshaji pamoja na mawazo ya watumiaji wa mabasi.

Taarifa hiyo inaonesha kuwa viwango vya nauli kwa mabasi ya kawaida yatumiayo barabara za lami imepanda kutoka sh. 26.6 hadi sh. 32.20 kwa kilometa kwa kila abiria, wakati mabasi ya yenye ubora wa wastani nauli yake itapanda kutoka sh. 40.7 hadi sh. 45.53 kwa kila kilometa huku nauli katika mabasi yenye hadhi ya juu (Luxury) kuanzia wiki ijayo nauli yake itapanda kutoka sh. 46.6 hadi sh. 51.64 kwa kila kilometa.

Taarifa hiyo inafafanua kwamba kwa upande wa mabasi yasiyotumia njia za lami kuna mabadiliko ya asilimia 23 yaliyofanyika ili kukabiliana na gharama za ziada kutokana na ubovu wa barabara.

Kulingana na mabadiliko hayo, taarifa hiyo ya SUMATRA inaeleza kwamba kiwango cha nauli kwa kilometa kwa mabasi yatumiayo barabara zisizokuwa za lami nauli zake zitapanda kutoka sh. 32.70 hadi sh. 37.80.

Hata hivyo taarifa inawaagiza wamiliki kutoza nauli kulingana na madaraja ya viwango vya mabasi yao, mabasi yote ya madaraja ya juu kuwa huduma zote mbadala kulingana na ubora wa mabasi yao vinginevyo wasitoze viwango hivyo.

Mbali na masharti hayo, SUMATRA pia inapiga marufuku kutumia wapiga debe, tiketi za mabasi yao kuuzwa kwenye ofisi rasmi na wamiliki wa mabasi hayo kuheshumu sheria na kanuni zote za usafirishaji barabarani.

Hatua hiyo ya SUMATRA imekuja baada ya Makao Makuu ya TABOA Mkoa wa Dar es Salaam na Tanga mwezi Desemba mwaka jana kuwasilisha maombi katika mamlaka hiyo wakiomba kuangaliwa upya kwa viwango vya nauli vinavyotozwa sasa, ili waweze kukabiliana na gharama za usafirishaji.

Katika maombi yao TABOA waliomba mamlaka hiyo kuongeza viwango vya nauli kati ya asilimia 16 na asilimia 185 za nauli ya sasa.

1 comment:

  1. Sumatra wanatoa mwelekeo wa nauli kulingana na classes za mabasi, sawa. Je walishafanya classification ya mabasi kwa madaraja? Ilitakiwa Sumatra hao wafanye hilo na kila basi liwe na sticker ya SUMATRA kuonesha daraja lake. Kwa hali ilivyo sasa itakuwa ni njia ya kuwaibia wananchi

    Suala la pili- Je wanaichi wa kawaida wanafahamu umbali wa routes zao kwa mfano mwananchi wa kawaida anayesafiri mara chache kati ya dar na Songea anafahamu umbali toka dar hadi songea? Ingebidi Sumatra wahakikishe kwamba umbali wa routes zote unakuwa kwenye tiketi za mabasi husika - hii ingesaidiwa wananchi kukokotoa nauli walizotozwa

    ReplyDelete