23 December 2010

Padre John kufunga kozi ya ukocha

Na Addolph Bruno

PADRE John Eyeble kutoka Chicago, Marekani kesho anatarajia kufunga kozi ya makocha wa ngumi ambayo inafanyika katika Uwanja wa ndani wa Taifa, Dar es Salaam.Kozi hiyo iliyoandaliwa na Shirikisho la
Ngumi Ridhaa Tanzania (BFT), ilishirikisha makocha 10 ambayo ilianza Desemba 14 mwaka huu.

Akizungumza Dar es Salaam juzi, Kaimu Rais wa (BFT), Meja Mstaafu Michael Changarawe ambaye pia ni mkufunzi wa kozi hiyo, alisema Padre John ambaye ni mdau wa ngumi tayari amewasili nchini.

"Padre John aliwahi kuwa mdau mkubwa wa mchezo huu hapa nchini katika mikoa ya Mwanza, Bukoba na mingine mingi, tumefurahi kuwa mgeni wetu katika shughuli hii kwa kuwa ni mdhamini mzuri," alisema Changarawe.

Changarawe aliongeza kuwa pamoja na mambo mengine, Padre John atakuwa na jukumu la kuwakabidhi vyeti wahitimu ambapo pia atazungumzia masuala mbalimbali kuhusu mchezo huo.

Aliwataja makocha waliohudhuria kozi hiyo kuwa ni Rajabu Mhamila 'Super D' wa klabu ya Ashanti, Lucas Hillary wa Ngome, Lucas Msomba wa Bandari, Junior Kimaro wa JKT, Miraji Mbagota, Moses Lema, Shime Mgeni, Mohamed Rajabu na Lupakisyo Mwakasiliba.

No comments:

Post a Comment