13 December 2010

Ofisa usalama adaiwa kuingilia uchaguzi

Na Patrick Mabula, Chato

MADIWANI wateule wa Hamashauri ya Wilaya ya Chato wamemtuhumu Ofisa Usalama wa Taifa wa Wilayani hiyo, Bw. Cusbert Madondola kuwa ameingilia uchaguzi wa kumpata mwenyekiti unaotarajiwa kufanyika wiki hii.Baadhi madiwani
hao wateule kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao hawakupenda kutajwa majina wamedai kuwa ofisa huyo ameingilia waziwazi na kutaka wamchague diwani mmoja anayemtaka yeye, hali iliyozua mgawanyiko mkubwa katika halmashauri hiyo.

Mbali na lawama hizo, pia wamedai kwamba ofisa huyo ambaye tayari amekanusha madai hayo, amekuwa akiwatishia kuwafungia shughuli zao binafsi baadhi ya madiwani kama hawatamchagua mgombea ambaye amekuwa akitaka apitishwe katika kikao chao ndani ya chama.

Mkuu wa Wilaya ya Chato, Bi. Khadija Nyembo alikiri kuwepo kwa malalamiko hayo ya baadhi ya madiwani huku akishangaa ofisa huyo kutuhumiwa wakati mapendekezo ya nani amepitishwa na vikao vya uteuzi bado hayajatolewa.

"Hata mimi nashangaa kwa kuwa masuala ya wanasiasa ni kuwaachia wenyewe na kama anajihusisha ni kinyume cha taratibu na nitamwita nimuulize hali hiyo, na hayo majina ya walioteuliwa najua hayajafika hapa wilayani kutoka vikao vya mkoa, yeye ameyatowa wapi," alihoji Bi.Nyembo.

Bw. Madondola alipoulizwa kuhusu madai hayo alikana kujihusisha na uchaguzi huo na kuonesha mshangao kwa madai dhidi yake akisema wengi walioshinda katika uchaguzi ni wapya ambao yeye hajawahi kukaa nao.

Alisema katika uchaguzi huo kumekuwepo na mipango ya baadhi ya watumishi wa halmashauri wakiongozwa na baadhi ya wakuu wa idara kumtaka diwani mmoja kama jina lake  litarudishwa kwa upande wa CCM, watahakikisha anapita kwa maslahi yao, ndiyo maana kumekuwepo na propoganda za kumchafua na kumhusisha na siasa hizo.

"Mimi sijihusishi na mchakato wa mwenyekiti wala sipigi kampeni kwa mgombea yeyote, kwanza wagombea wa nafasi ya mwenyekiti wa halmashauri wanaodaiwa kuwa majina yao yamerejeshwa kugombea nafasi hiyo sijayapata, japo nafahamu kuna walioomba, wako tisa.

"Kuwa upande wa CCM na walioteuliwa kupigiwa kura na vikao vyao vya ndani sijaona aliyepewa barua ya uteuzi, na mimi siwezi kuingilia uchaguzi wao. W wanaoingilia ni watumishi wa halmashauri kwa maslahi yao," alisema Madondola.

2 comments:

  1. Nice,Tabora
    Maafisa usalama wa Taifa wameshindwa kazi kwa hajui majukumu yao.Vema kikosi hicho kikuvunjwa na kuundwa upya na kupangiwa majukumu mpya ya kazi,Ndiyo maana hata uchaguzi mkuu uliingiliwa na kuvurugwa na watu wa usalama wa Taifa

    ReplyDelete
  2. nadhani walichodai CHADEMA dhidi ya matokeo ya uchaguzi mkuu 2010 sasa yanaanza kuonekana kwa watu walewale waliyotuhumiwa, ...."ukila nyama ya mtu utaendelea kula tu"

    ReplyDelete