Na Mwajuma Juma, Zanzibar
Timu za soka za Vietnam na Jamhuri ya Watu wa China, zimetumiwa mialiko na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kwa ajili ya kushiriki
mashindano ya kimataifa ya Kombe la Mapinduzi yatakayofanyika Zanzibar mwezi ujao
.
Timu hizo zimealikwa, ili
kupamba sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar yanayofikia kilele chake Januari 12
mwakani.
Kwa mujibu wa taarifa
iliyotumwa kwa vyombo vya habari jana iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Pili wa
Rais kupitia mwandishi wake, Othman Khamis ilieleza kuwa mwaliko huo umetolewa
na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya
Maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa Balozi Seif Ali Iddi, alipokuwa akizungumza
na Mabalozi wa nchi za Vietnam na Jamhuri ya Watu wa China kwa nyakati tofauti.
Balozi Seif alisema
Serikali tayari imeshaandika barua kwa nchi hizo na hatua hiyo, imefikiwa
kutokana na msimamo wa nchi hizo kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mara baada ya
kupata uhuru mwaka 1964.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa
Serikali imejiandaa kuzihudumia timu hizo kwa kutoa huduma za malazi, chakula
na usafiri wa ndani wakati zitakapokuwa nchini, huku nchi hizo zikitakiwa
ziwapatie tiketi za usafiri wa kwenda na kurudi Zanzibar.
Kwa upande wao mabalozi hao,
Nguyen Thanh Nam wa Vietnam na Lu youqing wa China wakizungumza na Balozi, Seif wameahidi
kulishughulikia ipasavyo suala hilo
la mualiko, ili kuona kwamba lengo lililokusudiwa la kutoa mwaliko huo
linafanikiwa vyema.
Mashindano
ya Kombe la Mapinduzi mwaka huu yatakuwa na makundi matatu, mawili yatakuwa
yakicheza Uwanja wa Amaan na kundi moja litacheza Uwanja wa Gombani, Pemba.
No comments:
Post a Comment