06 November 2013

LHRC WAMTAKA KAGASHEKI AJIUZULU



 Na Mariam Mziwanda
  Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimemtaka Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, ajiuzulu kutokana na agizo alilotoa kwa vyombo vinavyohusika kulinda maliasili za nchi kuwapiga risasi na kuwaua watu wote ambao watakutwa au kujihusisha na biashara ya nyara za Serikali.

  Mwanasheria wa LHRC, Bw. Harold Sungusia, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa kituo hicho, Dkt. Helen Kijo-Bisimba.
  Alisema ni kawaida ya viongozi wengi nchini kutopenda kuwajibika hivyo ni muhimu wakafahamu kuwa, hakuna aliye juu ya sheria ambapo kituo hicho kitapambana kulinda matakwa ya sheria za nchi si vinginevyo.
  "Wote waliohusika kuvunja haki za raia kwenye "Operesheni ya Tokomeza Ujangili" hawataachwa... operesheni hii ilikuwa ya mateso makubwa kwa watu mbalimbali kuumizwa vibaya, kupoteza maisha, nyumba za watu kuchomwa moto pamoja na kuuawa kwa mifugo.
  "Kituo kimepokea taarifa za vifo kutoka sehemu mbalimbali nchini... kimsingi hatutaogopa kumchukulia hatua za kisheria kiongozi yeyote ambaye atatumia nafasi aliyonayo kuvunja katiba ya nchi na haki za raia," alisema Bw. Sungusia.
  Aliongeza kuwa, mbali ya mauaji ya watu mbalimbali katika operesheni hiyo pia mifugo 190 ilipigwa risasi katika Kijiji cha Kegonga, Wilaya ya Tarime, mkoani Mara.
  Bw. Sungusia alisema operesheni hiyo ilifanyika kwa mfumo wa kutengeneza makambi maalumu ya kutesa watuhumiwa wa makosa ya ujangili ambapo kutokana na hali hiyo, kituo hicho wamelazimika kuwachukulia dhamana watuhumiwa 13.
  "Watu hawa walifikishwa katika Mahakama ya Bunda ambao walikamatwa na kuteswa katika kambi maalumu inayosimamiwa na Ofisa wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), ambaye alisaini hati ya kiapo cha kuwapeleka watuhumiwa mahakamani," alisema Bw. Sungusia.
  Aliongeza kuwa, watuhumiwa hao wameeleza walivyokamatwa kutokana na orodha iliyowasilishwa kwa Mkuu wa operesheni na kujikuta wametumbukia katika mateso ambayo yaliambatana na kumwagiwa pilipili na kutishiwa bunduki ili wakiri makosa.
  Alisema kituo hicho kinataka baadhi ya madaktari ambao kwa kiasi kikubwa wameonekana kupotosha ukweli wa sababu za vifo vya watu walioteswa kwa madai ya kuhusika na ujangili, kuchunguzwa na kuchukuliwa hatua za kinidhamu.
  Alifafanua kuwa, ipo haja ya Balozi Kagasheki kujiuzulu, Serikali kuizuia operesheni hiyo na watu walioathirika kulipwa fidia.
 "Tunatoa wito kwa viongozi kuongoza kwa kuzingatia misingi ya katiba, utawala wa sheria, haki za binadamu na kuepuka kutoa matamko ambayo yanakiuka haki za binadamu," alisema

No comments:

Post a Comment