27 November 2013

JK ‘AFUNGUKA’ MGOGORO ZIWA NYASA



  •  AWASILISHA VIELELEZO KWA WASULUHISHI WA MGOGORO


Na Penina Malundo
  Rais Jakaya Kikwete, amewasilisha utetezi wa Tanzania kwa jopo la Marais wastaafu wanaotafuta ufumbuzi wa mpaka wa Ziwa Nyasa, kati ya Tanzania na Malawi.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Bernard Membe, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema utetezi huo uliwasilishwa kwa Rais mstaafu wa Msumbiji Joaquim Chissano ambaye ndiye Mwenyekiti wa jopo hilo na Rais mstaafu wa Botswana, Bw. Festus Mogae.
Awali, viongozi hao wastaafu walifanya mkutano kama huo Blantyre, nchini Malawi ambapo juzi walisikiliza hoja za upande wa pili juu ya mgogoro huo.
"Katika mkutano huu, Rais Kikwete alitoa maelezo mazuri pamoja na vielelezo mbalimbali... utetezi wetu ulikuwa wa kisayansi hivyo hatuna hofu yoyote juu ya hili," alisema.
Bw. Membe alisema, leo anatarajia kwenda Maputo, nchini Msumbiji, kuwasilisha maelezo yaliyotolewa na Rais Kikwete mbele ya marais hao wastaafu.
Aliongeza kuwa, jopo la Wanasheria wa kimataifa bado linaendelea na kazi ya kufanya utafiti juu ya mgogoro huo kwani jambo hilo kwa kuliangalia ni dogo lakini ni kubwa.
Alisema kuwa mgogoro huu unaweza kuwa na tambo mbalimbali kati ya nchi moja na nyingine ingawa tambo hizo zinaweza kuleta athari kubwa kwa nchi hizo hivyo utafiti zaidi unahitajika.

No comments:

Post a Comment