04 October 2013

WAHARIRI WAPINGA KUFUNGIWA MAGAZETI



Na Mwandishi Wetu
  Jukwaa la Wahariri nchini (TEF), limepinga hatua ya Serikali kuyafungia magazeti ya Mwananchi (siku 14) na Mtanzania (miezi mitatu) na kudai adhabu hiyo imetolewa kutokana na sheria kandamizi ya magazeti ya mwaka 1976 inayolalamikiwa na wadau kwa miaka mingi.

Tamko hilo limetolewa kwenye kikao chao kilichofanyika Dar es Salaam jana ili kujadili uamuzi huo wa Serikali na kudai kuwa, hiyo ni moja ya sheria ambazo Tume ya Jaji Francis Nyalali, ilipendekeza ifutwe kwa sababu mbalimbali.
Sababu hizo ni pamoja na kukiuka misingi ya haki za binadamu, utawala bora, kwenda kinyume cha Katiba ya nchi pamoja na maazimio ya kimataifa ya haki za binadamu."Tunaungana na taasisi nyingine kupinga adhabu hii kwa magazeti ya Mwananchi, Mtanzania pia tukikumbushia kifungo cha gazeti la Mwanahalisi kwa sababu sheria iliyotumika haifai.
 "Hili si jambo la kuendelea kufumbiwa macho na jamii ambayo inafuata misingi ya kidemokrasia na utawala bora hivyo tunalaani kwa nguvu hatua hizi ambazo zimekiuka misingi hii ukizingatia Serikali ndiyo inayosimamia makubaliano ya kimataifa kuhusu uwazi katika uendeshaji wa Serikali," ilisema taarifa hiyo.
  Jukwaa hilo liliongeza kuwa, wanafahamu kuwa kuna kesi ya kupinga Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 iliyofunguliwa mwaka 2009 lakini ni jambo la bahati mbaya na kusikitisha sana kuwa hadi sasa, kesi hiyo haijaanza kusikilizwa kwa sababu ya kutopangiwa majaji.
"Tunapenda kutoa mwito kwa Mhimili wa Mahakama, kurekebisha kasoro hii na kupanga majaji wa kuisikiliza ili haki iweze kutendeka...kuchelewesha haki ni sawa na kunyima haki," iliongeza taarifa hiyo.
  Katika hatua nyingine, Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) , imedai kusikitishwa na uamuzi wa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuchukua hatua kali ya kulifungia gazeti lao.
  Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo, Bw. Tido Mhando, alisema kampuni hiyo ilionesha ushirikiano wa hali ya juu pale ilipoandikiwa barua ya kujieleza na kutoa ufafanuzi wa kweli juu ya habari zilizoandikwa na gazeti hilo. Habari hizo ni ile iliyohusu mishahara mipya ya watumishi wa Serikali na "Waislamu wasali chini ya ulinzi mkali wa polisi".

No comments:

Post a Comment