21 October 2013

VIJANA MTAJI WA SIASA KUELEKEA UCHAGUZI 2015



Adolf Mkono
‘‘ CCM wanaona jinsi wapinzani wao wanavyozidi kuimarika siku hadi siku na kujua matokeo halisi ya idadi za kura walizopata wao dhidi ya mpinzani wao na kuzifanyia kazi

  Harakati za kinyang'anyiro cha kiti cha urais mwaka 2015 kimekuwa kikivitesa vyama vya siasa na baadhi ya wanasiasa huku wananchi wakiendelea kutaabika kwa ukali wa maisha.Baadhi ya wanasiasa wamediriki kutamka wazi kuwa watagombea katika kiti hicho na kuzua malumbano kwa wananchi wao badala ya kusimamia shughuli za maendeleo kuwakomboa wananchi wao.

Ni rahisi kutambua kuwa harakati za chini na zingine za wazi kwa vyama hivyo kikiwemo CCM kama chama tawala tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu 2010, inatoa maana moja tu kubwa kuweka mazingira sawa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Hatua hii ya kila chama kuhangaika mapema kiasi hiki huku ikiwa ni nusu ya kipindi kingine cha uchaguzi ni ishara nzuri kwa ukuaji na kukubalika kwa mfumo wa vyama vingi kwa sehemu kubwa ya Watanzania tofauti na miaka ya nyuma.
Hali hii inaashiria kuwa uchaguzi ujao utakuwa mgumu kwa pande zote kutokana na maandalizi yanayoendelea sasa.Wananchi wamefunguka na kufuatilia yanayoendelea, hivyo ni wakati mwafaka kwa serikali pia kulinda amani iliyopo kwa gharama yoyote ili kuepusha migogoro baada ya uchaguzi ambayo mwisho wa siku hurudisha nyuma maendeleo.
Wakati huu tunapoendelea na mchakato wa katiba mpya ni vizuri sasa wananchi wakasikilizwa kile wanachokitaka kwani wengi wao wamekuwa wakitoa maoni kuhusiana na suala hilo.Harakati zinazoendelea kwa vyama vya siasa na hapa hebu tuanze na CHADEMA chama ambacho katika uchaguzi wa rais 2010 kilimsimamisha Dkt.Wilbroad Slaa kama mgombea hatua iliyomtoa katika nafasi yake ya ubunge.
Matokeo yake ikawa ni kuwa nje ya uwakililishi wa wananchi atakisaidia vipi chama chake hasa ikizingatia njia aliyoitumia kukijenga ilikuwa ni kupitia bunge alikoibua madudu ya EPA na RICHMOND na kusababisha matokeo mabaya ya CCM kwa uchaguzi wa mwaka 2010.
  Waswahili husema, adui yako muombee njaa! Na kama CCM walifuata kanuni hiyo ukweli ni kwamba watakuwa wanakosea na kama hawaamini watakuja kugundua hilo wakiwa tayari wamechelewa.Sidhani kama wanaweza kujisahau kiasi hicho, imani yangu ni kuwa wanafuatilia kila hatua inayoendelea ndani ya chama hicho ndio maana hawataki kubweteka hata kidogo.
  Moja ya kitu walichokigundua CHADEMA ni udhaifu wa uongozi ndani ya chama hicho hasa ngazi za matawi, kata, wilaya na majimbo, kazi ambayo Dkt.Slaa kama katibu mkuu wa chama amekuwa akiifanya ukaguzi na kuhakikisha anaweka uongozi imara kwa ngazi hizo ambayo tayari imekamilika zaidi ya wilaya 150.
  Kwa yoyote atakayeteuliwa na CHADEMA kupeperusha bendera yake katika nafasi ya urais ataingia kwenye kinyang'anyiro huku akiwa na imani kubwa kuwa kweli nyuma yake ana 'makamanda' wa uhakika kama wao wanavyopenda kujiita na ikumbukwe kuwa kwa kazi inayoendelea ni vigumu CCM kupata viti vya bwerere kama ilivyopata awali.
  Hali ikiwa hivi upande wa chama kikuu cha upinzani kwa sasa CHADEMA, CCM nao hawajalala japo mbinu zao ni tofauti kidogo na wenzao wa upinzani maana kama ni kuimarisha ngazi za chini tayari mwasisi wa chama hicho upande wa bara Hayati Baba wa Taifa Julius Nyerere aliifanya.
  Kwa matukio ya hivi karibuni yanayoendelea ndani ya chama tawala na serikali yake ni vigumu kuamini kama yanatokea kwa bahati mbaya ama kusudi.Kuna watu wanabeza uteuzi wa sekretarieti iliyopo ila ukweli ni kwamba inajua kucheza na rika la vijana ambalo ndilo tishio kwa ustawi wa chama chochote.
  Hivi karibuni tulisikia CCM wakianzisha kanda maalum upande wa wanafunzi wa elimu ya juu eneo lililotumiwa na CHADEMA miaka michache iliyopita na kuleta ufanisi mkubwa kwa matunda ya akina Zitto, Mnyika na Mdee, ambao tayari kwa sasa ni nguzo za chama hicho.
  Kuna dhana kwamba sekretarieti hiyo inaendeleza mpasuko wa makundi ya chama hicho moja likiwa lile la watuhumiwa wa ufisadi na wapinga ufisadi ndani ya CCM.Katika hili, ukweli ni kwamba kundi lisilopenda maendeleo ya chama ni vigumu kwao kukiacha chama chao tofauti na vijana ambao kuhamia upinzani kwao ni kitendo cha kishujaa na zaidi ya hapo tofauti zao zitafikia mwisho baada ya CCM kumpata mgombea wake wa urais 2015.
  Watuhumiwa wa ufisadi wanaweza kuwa na tofauti na mapungufu mengi lakini tukumbuke CCM kuondoka madarakani ni vigumu kwao kubaki salama japo kuna wanaoonekana kama vinara wa ufisadi lakini ukweli ni kwamba hapo hakuna aliye msafi kiasi cha kuamini kwamba nje ya serikali ataendelea kuwa salama si kwa sababu viongozi wa sasa ni mafisadi la hasha!
  Bila shaka CCM wanaona jinsi wapinzani wao wanavyozidi kuimarika siku hadi siku na kujua matokeo halisi ya idadi za kura walizopata wao dhidi ya mpinzani wao na kuzifanyia kazi.Na kama hali itaendelea kuwa hivyo ya kushindwa kuisambaratisha CHADEMA itabidi sasa CCM wajisalimishe kwa mtu mmoja ndani ya chama hicho ili kuibuka kama mgombea binafsi kwa ajili ya kupunguza kura za mpinzani wake.
  Tukiendelea na mchakato wa katiba mpya, ni wakati wa kuyarekebisha yote yanayokinzana na vyama vingi kama, matokeo ya urais kupingwa mahakamani.Hii ni moja ya sababu iliyokuwa ikichangia msukumo wa madai ya katiba mpya kwa wapinzani. Sasa hivi CCM ndo wameanza kulipigia chapuo jambo hili katika mchakato wa katiba mpya.
  Katiba iliyopo sasa rais aliyepo madarakani alikuwa akiingia kwenye kinyang'anyiro cha nafasi hiyo huku akiwa bado ndiye rais wa nchi ukiachilia yeye kuvunja Bunge na baraza lake la mawaziri hili linatakiwa kutazamwa ili kuondoa utata.
  Wapo waliokuwa wanaona ni vyema serikali ikawa chini ya muhimili mmojawapo kati ya Bunge au mahakama japo kila sehemu ina changamoto zake, ukisema dola kwa kipindi hicho iwe upande wa mahakama kuna uwezakano wa kuibuka hoja mkuu wa muhimili huo kuwa mteule wa rais na kama litakuwa Bunge.
  Pia, kuna hoja ya spika kuwa sehemu ya chama tawala, wakati hayo yote yakihitaji majadiliano tayari CCM wameisha kubali matokeo kupingwa mahakamani, inawezekana baadhi ya changamoto zikapatiwa ufumbuzi ila ni ngumu madai yote kupita kama yanavyopendekezwa na wapinzani.
  Kiongozi mwenye nia thabiti ni yule anayeumia kwa ajili ya wananchi wake, ni wakati mwafaka sasa kutafuta njia ya kuwatoa wananchi katika hali ya ugumu wa maisha na kupanda kwa bidhaa ili kuongeza uzalishaji katika taifa.


.

No comments:

Post a Comment