23 October 2013

UHABA WA WATAALAMU KUTAWALA MKUTANO MKUU NAIROBI KENYA



Na Anne Kiruku, EANA
  Mkutano wa siku tatu unaojumuisha wataalamu wa vyuo vikuu vya umma vya Afrika Mashariki na watendaji wakuu wa sekta binafsi, unatarajiwa kujikita zaidi kuhusu uhaba wa wataalamu na mahitaji ya soko la ajira.

  Mkutano huo wa Jukwaa la Wasomi na Sekta Binafsi na Maonesho ya mwaka 2013 utakaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Jomo Kenyatta Kenya, utawajumuisha wadau kutoka nchi tano wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Nchi hizo ni pamoja na Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda na Burundi.
Mkutano huo uliochini ya kauli mbiu, "Kuunganisha wasomi na sekta binafsi kupitia sekta ya umma,'' unawaleta pamoja wataalamu wasomi waliobobea katika nyanja mbalimbali na wafanyabiashara waandamizi, watajadili masuala yanayogusa pande zote za washiriki wa mkutano huo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Biashara la Afrika Mashariki (EABC), Andrew Luzze aliliambia Shirika Huru la Habari la Afrika Mashariki (EANA) kwamba sekta binafsi vyuo vikuu watajadiliana kwa pamoja mkakati wa kushughulikia suala la ukosefu wa ajira na kukosekana kwa ujuzi unaotakiwa kwa wahitimu wa vyuo vikuu katika Kanda hiyo ya Afrika Mashariki.
  "Wanafunzi wanasema hakuna kazi.Sekta binafsi inasema wana kazi, lakini ujuzi unaohitajika na sekta binafsi si ule ambao wahitimu husika wanao,'' alisema.
  Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Katibu Mtendaji wa Baraza la Vyuo Vikuu vya Afrika Mashariki, Prof. Mayunga Mkunya amekubaliana na maoni hayo.
  Tatizo hilo alisema, lipo katika nchi zote tano wanachama wa EAC.''Tunataka kujadili namna ya kufanya marekebisho ya mitaala ya kufundishia ambao utawezesha kuzalisha wahitimu wenye ujuzi na mwelekeo.''
  Luzze alisema washiriki wapatao 250 wameshathibitisha kuhudhuria. Kutakuwepo na watakaofanya maonyesho 77 kutoka vyuo vikuu na sekta binafsi.
  

No comments:

Post a Comment