23 October 2013

PAC YATAKA WIZARA YA ELIMU IKAGULIWE



  Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), imemwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kufanya ukaguzi wa mahesabu haraka iwezekanavyo katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ili kuondoa sintofahamu ya mahesabu yake, anaripoti Anneth Kagenda.

  Agizo hilo lilitolewa Dar es Salaam jana na Kaimu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw. Gaudence Kayombo, alipokutana na watendaji wa Wizara hiyo akiwemo Katibu Mkuu, Profesa Sifuni Mchome.“Hatusemi fedha imeliwa hapana ila tumeagiza ukaguzi ufanyike mara moja ili kubaini ukweli wa hesabu zenu...pamoja na kwamba majibu ya Katibu Mkuu yanaridhisha, lengo letu ni kupata majibu ya kueleweka,” alisema Bw. Kayombo na kuongeza;
  “Mfano Wizara imetoa milioni kadhaa kwenda Mkwawa au katika vyuo na taasisi za elimu... tunachotaka tukiangalia taarifa za huko tukute zinafanana zisikinzane lakini tunaamini baada ya CAG kufanya ukaguzi wake tutabaini tatizo liko wapi,” alisema.
  Aliongeza kuwa, uhamishwaji fedha kwenda kwenye taasisi bado haujaeleweka na unakinzana na kutoa mfano kuwa, Wizara hiyo imepeleka fedha ADEM Bagamoyo ambazo zinaonesha sh. milioni moja lakini taasisi husika itasema ilipokea zaidi au pungufu.
  Bw. Kayombo alisema umefika wakati wa watendaji katika wizara hiyo, kuhakikisha wanaisaidia Wizara iweze kufanya shughuli zake vizuri badala yake wamekuwa wakimwangusha Katibu Mkuu ambaye anaonekana kuwa na majibu ya uhakika pale anapotakiwa kufanya hivyo.
  Alisema watendaji hao, mwaka 2012 walipewa mambo matano ya kufanya lakini cha kushangaza wamefanya jambo moja ambalo ni kutembelea Shule ya Sekondari ya Miono, iliyoko Mjini Bagamoyo, mkoani Pwani na taarifa imeonesha shule hiyo inahitaji uzio.
  “Shule hii iko karibu na Mbuga hivyo tulishauri iwekwe uzio, hilo tu ndiyo walilofanya lakini tuliwaagiza waangalie ada za wanafunzi wa vyuo vya juu jambo hilo bado halijafanyika,” alisema.Aliongeza kuwa, Bodi ya Mikopo pia ilitakiwa kutoa maelezo ya utoaji mikopo kwa wanafunzi, kuangalia uwezekano wa kujiendesha yenyewe badala ya kuitegemea Serikali badala yake bodi hiyo ilikwenda na mkakati wake.
  Prof. Mchome, alipoulizwa juu ya mkanganyiko wa fedha hizo alisema; “Nadhani hili ngoja likafanyiwe kazi lakini ninachojua hakuna fedha iliyoliwa,” alisema. Akizungumzia suala la ukusanyaji mikopo, alikiri bado jitihada kubwa zinahitajika katika ukusanyaji huo.

No comments:

Post a Comment