16 September 2013

YANGA YAIKATIA RUFAA MBEYA CITY



  • YALIA KUHUJUMIWA MECHI YA J'MOSI

Na Hamis Miraji, Mbeya
UONGOZI wa Klabu ya Yanga, jana umewasilisha barua yao ya rufaa katika Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), ikitaka mechi dhidi ya Mbeya City irudiwe kutokana na kufanyiwa hujuma
.Katika mechi hiyo ya Ligi Kuu Tanzania Bara, iliyochezwa Jumamosi Uwanja wa Sokoine jijini hapa timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1.
Kabla ya mechi hiyo kuchezwa mashabiki wanaodhaniwa wa Mbeya City walivamia basi lililobeba wachezaji wa Yanga na kusababisha kuvunjika kioo cha basi hilo.
Akizungumza jijini hapa jana Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto alisema timu yake ilifanyiwa vurugu na kusababisha wachezaji kucheza kwa woga, kitu ambacho kimesababisha wacheze chini ya kiwango na kutoka sare hiyo.
"Wachezaji walitoka kwenye mchezo kwa kufikiria kufanyiwa vurugu na kushindwa kufanya kile walichotakiwa jambo lililowafanya kutoka sare ya bao 1-1," alisema Kizuguto.
Alisema licha ya kushambuliwa ndani ya uwanja, hata walivyotoka uwanjani baada ya mechi kumalizika mashabiki wa Mbeya City waliendelea kushambulia gari la viongozi wa Yanga aina ya Noah.
Katika hatua nyingine, uongozi wa Mbeya City umeiomba radhi Yanga kwa vurugu zilizotokea katika mechi hiyo iliyokuwa na upinzani mkubwa.
Akizungumza jijini hapa jana Katibu Mkuu wa Mbeya City, Emmanuel Kimbe alisema wanaiomba radhi Yanga kwa matatizo yaliyojitokeza katika mechi hiyo.
"Sisi kama viongozi tunaomba radhi kwa wenzetu wa Yanga kwa yaliyotokea siku ya mchezo wetu wa Ligi Kuu," alisema Kimbe.
Kimbe alisema kitendo kilichofanyika si cha kiungwana, hivyo wanakemea kwa nguvu zote.
Alisema wamewapa majukumu vyombo vya dola kwa atakayebainika atachukuliwa hatua kali za kisheria

No comments:

Post a Comment