07 September 2013

USHAHIDI KESI YA MHASIBU OUT WAANZA KUTOLEWA



Na Rehema Mohamed
UPANDE wa mashtaka katika kesi ya utakatishaji fedha ambayo inamkabili aliyekuwa Mhasibu wa Chuo Kikuu Huria nchini (OUT), Engels Mrikarika, umeielezea Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jinsi mshtakiwa alivyokuwa akimuingizia fedha mpenzi wake Rose Maungu.

Wakili wa Serikali Prosper Mwangamila, aliyasema hayo jana mahakamani hapo mbele ya Hakimu Augustina Mbando, wakati akiwasomea maelezo ya awali washtakiwa hao.Alidai katika vipindi tofauti kati ya Julai mosi 2009 na Aprili 30,2011 jijini Dar es Salaam, Mrikarika kwa makusudi aliandaa nyaraka za malipo ya mishahara ya wafanyakazi wa chuo hicho na kuingiza jina la Maungu na wengine watano.
Aliongeza kuwa, wakati huo Maungu alikuwa akifanya kazi Chuo cha Biashara (CBE), Tawi la Dar es Salaam kama Katibu Muhtasi lakini Mrikarika aliingiza jina hilo akionesha ni mfanyakazi wa chuo hicho hivyo anastahili kulipwa wakati si kweli.
I l i d a iwa ms h t a k iwa Mrikarika alipeleka nyaraka hiyo katika Benki ya NBC, tawi la Cooparate na kutoa ma e l e k e z o kwa b e n k i hiyo ifanye malipo kutoka akaunti 0111030002560 ya chuo hicho kwenda akaunti 0150205110500, 019201046241 za Benki ya CRDB Tawi la Kichewe akimuingizia Maungu sh. milioni 68.
Mwangamila alidai kuwa, Maungu alizitoa fedha hizo, kuzifanyia matumizi binafsi na nyingine kuziingiza katika biashara ya duka la vifaa vya ofisini liitwalo Judiana Stationery ambalo wanashirikiana na mpenziwake Mrikarika ili kuficha chanzo cha fedha hizo ionekane zilipatikana kwa njia ya biashara.
Alisema katika maelezo ya onyo aliyotoa polisi, Maungu alikiri kutokuwa mtumishi wa chuo hicho ingawa alikuwa akipokea malipo kutoka akaunti 011103000250 NBC kutoka OUT.
Hakimu Mbando alipowahoji washtakiwa hao juu ya maelezo hayo, waliyakana pamoja na uhusiano wa kimapenzi. Mwangamila aliieleza mahakama hiyo kuwa ili kuthibitisha mashtaka dhidi ya washtakiwa hao, wanaomba wapangiwe tarehe ya usikilizwaji ili walete mashahidi pamoja na vielelezo mbalimbali.
Hakimu Mbando aliahirisha shauri hilo hadi Septemba 19 mwaka huu, kwa ajili ya usikilizwaji.

No comments:

Post a Comment