07 September 2013

PINDA ‘AFUNGUKA’



  •   AWATAKA WAPINZANI KUTAMBUA DHAMANA YAO
  • CHADEMA,CUF WAINGIA BUNGENI WAONDOKA
Mariam Mziwanda na Rehema Maigala
WAZIRI Mkuu, Bw. Mizengo Pinda, jana aliahirisha Mkutano wa Bunge la 12, mjini Dodoma, ambalo lilipitisha Miswada mitatu ukiwemo wa Sheria ya Taifa ya Umwagiliaji wa mwaka 2013.Miswada mingine ni Muswada wa Sheria wa Vyama vya Ushirika wa Mwaka 2013 na Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka 2013.

Katika hotuba yake, Bw. Pinda aliwaomba wabunge kutoka upinzani watambue umuhimu wa chombo hicho na kutambua dhamana waliyopewa na Watanzania wanaowawakilisha.Alisema wabunge hao wanapaswa kutumia busara na kuona umuhimu wa kushiriki vikao vya maamuzi kwa masilahi ya Watanzania na Taifa kwa ujumla.
 Akizungumzia vita dhidi ya dawa za kulevya nchini, alisema mapambano hayo hayawezi kukomeshwa na nchi moja hivyo yatafanikiwa kama nchi zote duniani zitaungana ili kudhibiti biashara hiyo kwani wauzaji, wasafirishaji na watumiaji wanaishi kwenye jamii na baadhi yao wanafahamika.
“Nitoe wito kwa wananchi wote, kushirikiana na vyombo vya Ulinzi na Usalama kuwafichua na kutoa taarifa za watu ambao wanajihusisha na biashara hii... Serikali itaendelea kuchukua hatua stahiki kwa watakaobainika,” alisema Bw. Pinda.
Ujenzi miundombinu ya gesi
Bw. Pinda alisema, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya kitaifa ya kipaumbele katika sekta ya Nishati kupitia Mfumo Mpya wa ‘Tekeleza Sasa kwa Matokeo Makubwa’ (Big Results Now).
Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa bomba la gesi asilia kutoka Mtwara-Lindi hadi Dar es Salaam na kujenga mitambo miwili ya kusafisha gesi hiyo katika maeneo ya Mnazi Bay-Madimba (Mtwara) na Kisiwa cha Songo Songo (Lindi).
Hadi sasa meli nne kati ya 12, zimewasili nchini zikiwa na shehena ya vipande 16,623 vya mabomba ambayo yameanza kusambazwa katika maeneo husika ambayo yatawezesha ujenzi wa bomba wa umbali wa kilomita 194 kati ya kilomita 532.Aliongeza kuwa, ujenzi wa nyumba za wafanyakazi wa mradi unaendelea ambapo kazi ya kulaza bomba kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam inategemewa kukamilika Juni 2014 na mradi wote utakamilika Desemba 2014.
Bomba hilo la gesi linatarajiwa kusambaza gesi katika maeneo ya Mtwara, Lindi, Kilwa, Somanga Fungu, Mkuranga, Dar es Salaam na maeneo mengine ya Tanzania kwa matumizi mbalimbali.Baada ya kipindi cha maswali na majibu, alisimama Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Angellah Kairuki kuwasilisha hoja za Serikali kuhusu muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka 2013.
Kabla Bi. Kairuki hajaanza kuzungumza, wabunge wa upinzani kutoka vyama vya CHADEMA na CUF walisusia kikao cha Bunge na kutoka nje ya ukumbi huo.
Kitendo hicho kilisababisha baadhi ya wabunge kuomba mwongozo juu ya vurugu zilizotokea bungeni juzi ambapo Mbunge wa Simanjiro, mkoani Manyara, Christopher Ole Sendeka, akihoji msamaha wa kiti cha Spika kwa wabunge waliohusika na vurugu hizo.Alisema kitendo cha Mbunge wa Mbeya mjini, Bw. Joseph Mbilinyi (CHADEMA), kuchukua sheria mkononi na kumpiga askari wa Bunge ni cha fedheha.

No comments:

Post a Comment