16 September 2013

MUHONGO AFICHUA SIRI MAPINDUZI YA UCHUMI



Na Suleiman Abeid, Kahama
SERIKALI imedhamiria kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi ili kuiwezesha Tanzania kuwa na uchumi unaotoa ajira kwa vijana na kuongeza pato la mwaka kwa wananchi tofauti na sasa.

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, aliyasema hayo juzi, wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na wakazi wa vijiji mbalimbali vilivyopo Wilaya za Kahama, Mkoa wa Shinyanga na Bukombe mkoani Geita alipokuwa katika ziara ya kukagua utekelezaji wa mradi wa upelekaji umeme vijijini (REA).
Alisema kipaumbele cha Wizara hiyo kwa sasa ni kuhakikisha nchi inapata umeme wa uhakika ambao utatumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na matumizi ya nishati ya gesi ili kuleta mapinduzi kwenye sekta ya viwanda.
Aliwataka wakazi wa vijijini wenye tabia ya kwenda mahakamani ili kudai walipwe fidia ya nguzo za umeme kupita katika mashamba yao waache mara moja kwani inachelewesha utekelezaji wa mradi huo mkubwa wenye lengo la kuwakomboa katika umaskini.
"Serikali imedhamiria kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi katika sekta ya nishati ya umeme kupitia kauli mbiu ya uchumi na maendeleo, juhudi hizi zitafanikiwa kama Watanzania wenyewe tutaunga mkono jambo hili.
"Tunataka ifikapo 2015, kuwepo ongezeko kubwa la Watanzania wanaotumia umeme angalau asilimia 30, Shirika la Umeme nchini (TANESCO), limejipanga kuhakikisha tunafikia lengo la kuzalisha megawati 3,000 ambazo tutaweza kuuza nje ya nchi na kuiwezesha nchi yetu kutekeleza miradi yake mingi ya maendeleo," alisema.
Prof. Muhongo aliwahadharisha mawakala waliopewa kazi ya kusambaza umeme vijijini, kuhakikisha wanafanya kazi hiyo kwa kuzingatia muda uliomo katika mikataba na wakala ambaye atazembea, ataondolewa na kupewa mwingine.

No comments:

Post a Comment