11 September 2013

MKEMIA ASITISHA VIBALI VYA KUINGIZA KEMIKALI



Na Charles Mwakipesile, Mbeya
SERIKALI imetangaza kufuta vibali vya wanaofanya kazi ya kuingiza kemikali nchini kwa ajili ya kudhibiti matumizi yake ikiwemo tindikali ambayo imekuwa ikitumika kwa ajili ya uhalifu na kutishia maisha ya Watanzania.

Mkemia Mkuu wa Serikali, Prof. Samwel Manyele alitangaza uamuzi huyo jana wakati akizungumza na Dawati la Mkoa la Ukatili wa Kijinsia katika ofisi ya Mganga Mkuu mkoani Mbeya.
Alisema kuwa, Serikali imekuwa ikipambana na uingizaji holela wa kemikali ambao ndiyo umekuwa chanzo cha kubadili matumizi ya kemikali ambazo zimekuwa zikitumika ovyo katika machimbo na wahalifu ambao wamekuwa wakitumia kwa ajili ya kuangamiza maisha ya Watanzania.
"Tatizo kubwa tulilolipata ni kutokana na waingizaji, wasafirishaji, watumiaji kubadili matumizi ya kemikali na kuishia kuzifanya ni sehemu ya silaha za kuangamiza Watanzania, hali ambayo sisi kama wadhibiti hatuwezi kukubali iendelee, sasa tumefuta vibali vyote na wanaotaka wataomba upya ili tuweze kupata nafasi ya kuwabaini wanaopotosha matumizi," alisema.
Hata hivyo, Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Dkt. Agnes Buto alisema kuwa ujio wa Mkemia Mkuu unatoa majibu ya maswali mengi waliyokuwa nayo kuhusiana na utendaji wa ofisi hiyo ambayo imekuwa ni muhimu sana kwa kazi zao wakati wote.

No comments:

Post a Comment